Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

JB Fuel yatoa msaada vifaa kujikinga na corona kwa watoto wenye ualbino

Wed, 22 Apr 2020 Chanzo: --

Kampuni ya Jb Fuel ya mjini Bariadi mkoani hapa, imetoa msaada wa vifaa mbalimbali vya kujikinga na ugonjwa wa homa ya mapafu unaosababishwa na virusi vya corona katika Kituo cha kulelea watoto wenye mahitaji maalumu cha Bikira Maria.

Kituo hicho chenye idadi kubwa ya watoto wenye ualbino, wakiwamo wengine wenye ulemavu mbalimbali na yatima kilichopo mjini Lamadi Wilaya ya Busega, kimepokea msaada huo wenye thamani ya Sh milioni mbili.

Akikabidhi msaada huo leo Jumatano Aprili 22, kwa Mratibu wa kituo hicho, Mkurugenzi wa Kampuni hiyo Lucy John amesema mbali na vifaa hivyo, kampuni yake imetoa chakula kwa ajili ya watoto wa kituo hicho.

Aidha amevitaja hivyo vifaa vya kujikinga na ugonjwa huo, ni pamoja na ndoo za kunawia mikono, pamoja na vitakasa mikono vitakavyowasaidia watoto hao kujikinga na virusi hivyo ambavyo vimekuwa hatari duniani.

“Binafsi kwa dhati ya moyo wangu nimeamua kuungana na serikali kuhakikisha hakuna maambukizi zaidi ya ugonjwa wa corona ambayo yanaweza kutokea hasa katika mkoa wetu,” amesema Lucy.

Naye mratibu wa kituo hicho, Sister Helena akipokea msaada huo amesema kuwa kituo hicho chenye jumla ya watoto 71 kinahudumia watoto kutoka mikoa mbalimbali wakiwamo walioachwa na wazazi wao wakati wa kujifungua.

Sister Helena amemshukuru Mkurugenzi wa Kampuni hiyo kwa kuwajali watoto wa kituo hicho hasa katika kipindi hiki cha ugonjwa huo hatari, ambapo ameeleza utawasaidia sana watoto hao na wafanyakazi kuweza kujikinga.

Chanzo: --