Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) imeweka mipango ya kupandikiza figo kwa wagonjwa zaidi 200 kwa mwaka.
Hayo yamebainishwa leo Dar es Salaam na Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano MNH, Aminiel Aligaesha mara baada ya kuruhusiwa wagonjwa wawili ambao wamepandikizwa figo April mwaka huu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili.
Amesema katika mpango wa muda mfupi, kila mwezi hospitali hiyo itapandikiza figo wagonjwa watano, hivyo kwa mwaka itakuwa imefanikiwa kupandikiza figo wagonjwa 60.
“Kila siku mgonjwa mmoja atapandikizwa figo, kwa wiki tutakuwa tumepandikiza figo wagonjwa watano, kwa mwezi wagonjwa 20 na kwa mwaka tutafanikiwa kupandikiza figo wagonjwa 240,’’ amesema Aminiel.
Naye Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Figo MNH, Dkt. Onesmo Kisanga amesema takribani wagonjwa 800 nchini wanasubiri huduma ya upandikizaji figo na kati ya hao 50 tayari wameandaliwa.