Dar es Salaam. Hospitali ya Taifa Muhimbili- Mloganzila kwa mara ya kwanza imefanya upasuaji wa kuondoa vivimbe katika mishipa ya damu kwenye ubongo.
Upasuaji huo unaofahamika kitaalam kama Cerebral aneurysms umefanyika kwa Cosila Tambila (62) na kuifanya Mloganzila kuwa hospitali ya pili ya umma Tanzania kutoa huduma hiyo.
Upasuaji huo uliofanyika kwa saa sita umefanywa na madaktari bingwa wa upasuaji ubongo wakiongozwa na daktari bingwa mshauri wa upasuaji ubongo na mishipa ya fahamu Profesa Huh Seong kutoka Yonsei, Korea Kusini.
Daktari bingwa wa upasuaji wa ubongo Raymond Makundi amesema licha ya ugonjwa huo kutozungumzwa mara kwa mara umekuwa ukiwasumbua watu wengi.
Amesema kufuatia hali hiyo ni asilimia 50 pekee ya wagonjwa wanaofika hospitali kwa ajili ya kupata matibabu sahihi na wengine hupata matibabu mengine wakidhaniwa kuwa na kiharusi kutokana na kuchelewa kufika hospitali.
Amezitaja dalili za ugonjwa huo ni pamoja na maumivu makali ya kichwa, kupoteza uwezo wa kuona na kupoteza fahamu.
Pia Soma
- Watumishi wa TRA Geita wadakwa wakiomba rushwa ya Sh100 milioni
- Polisi Geita yawadaka watatu wakijifanya maofisa usalama
“Nilianza kuumwa kichwa tangu mwezi wa tatu nilikwenda hospitali halikuonekana tatizo wakanipeleka Muhimbili huko ndiko nilifanyiwa vipimo na kuonekana na tatizo hili.”
“Nashukuru kwa sasa maumivu ya kichwa yameisha na hatimaye leo nimeruhusiwa kurudi nyumbani,” amesema Tambila
Kwa upande wake Naibu Mkurugenzi wa hospitali hiyo, Julieth Magandi amesema Mloganzila imejipanga kuwekeza kwenye matibabu hiyo ili itolewe kwa uhakika.
“Lengo letu ni kutoa matibabu ya kibingwa na tunaendelea kujiimarisha kufanikisha hilo, tunawekeza kwenye vifaa na watalaa wa matibabu haya na kufanikiwa kwa upasuaji huu kumetupa furaha iliyoje,” amesema Dk Magandi