HOSPITALI ya Rufaa ya Kanda ya Bugando wilayani Nyamagana ipo katika mkakati wa kutafuta Sh bilioni 5.4 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa jengo la saratani katika hospitali hiyo.
Kaimu Mkurugenzi wa hospitali hiyo, Dk Lufingo Mwaipopo juzi alisema wameshaanza ujenzi wa wodi ya saratani na itakuwa na vitanda 120 lakini wanakabiliwa na changamoto ya uhaba wa fedha.
Alisema katika kukabiliana na hali hiyo watumishi wa hospitili hiyo wamekubaliana kuwa sehemu ya kuchangia fedha za kukamilisha ujenzi hao.
“Watumishi tumekubaliana tuwe sehemu ya michango, tutachangia Sh milioni 250 kutoka vyanzo vyetu vya mapato ambavyo ni mishahara yetu,” alisema.
Dk Mwaipopo alisema katika kukamilisha ujenzi huo hospitali hiyo imeona vyema ichangie Sh bilioni moja na serikali imechangia Sh bilioni 1.7 lakini mpaka sasa wanahitaji Sh bilioni 5.4 ili kukamilisha ujenzi huo.
Kwa upande wake, Mbunge wa Nyamagana, Stanslaus Mabula alisema katika kuisaidia hospitali hiyo atazungumza na wabunge wenzake wa majimbo na wa viti malumu kutoka mikoa ya Kanda ya Ziwa ili waweze kuchangia ujenzi huo wa wodi ya saratani haraka.
Meya wa Jiji la Mwanza, Sima Costantine aliishukuru Hospitali ya Bugando kwa kuendelea kusaidia wananchi kwa kutoa misamaha ya huduma ya matibabu.