Dar es Salaam. Hospitali ya Rufaa ya Kanda Bugando (BMC) ipo mbioni kuanzisha taasisi ya moyo ili kuweza kuhudumia wananchi wa Mikoa ya Kanda ya Ziwa.
Mkurugenzi wa hospitali hiyo Profesa Abel Makubi amesema taasisi hiyo itakuwa na majengo mawili ya ghorofa 10 na 15.
Profesa Makubi amesema Sh59 bilioni zitatumika katika ujenzi wa majengo hayo.
"Serikali ya awamu ya tano imedhamiria kwa dhati kutoa huduma zote za kibingwa na bobezi hapa nchini, hii itapunguzia mzigo serikali na wizara kupeleka wagonjwa nje ya nchi vilevile wananchi wa kanda hii kunufaika na huduma za moyo huku huku," amesema.
Kwa upande wa watumishi Profesa Makubi amesema wameweza kuongeza wataalam wa fani mbalimbali kutoka ndani na nje ya nchi wakiwepo wauguzi, madaktari, madaktari bingwa na bobezi na hivyo kufanya kazi ya utoaji huduma katika idara zote bila kuteteleka.