Shirika la Afya Duniani (WHO) linatazamiwa kufanya mkutano maalum leo Ijumaa kuhusu aina mpya ya virusi vinavyoenea kwa kasi nchini Afrika Kusini.
Wataalamu huko Geneva wataamua ikiwa kuna haja ya kuweka mkazo kuhusu wasiwasi wa virusi hivyo. Afisa mkuu wa WHO alisema inaweza kuchukua mpaka wiki kubaini ikiwa idadi kubwa ya mabadiliko ya chembe za urithi za kirusi hicho ina athari kwa ufanisi wa chanjo zilizopo.
Hilo linakuja wakati Uingereza imeweka marufuku ya muda kwa safari zote za ndege kutoka Afrika Kusini na nchi tano jirani. Hakuna visa vilivyogunduliwa nchini Uingereza. Wataalamu wa Afrika Kusini wanasema kirusi hicho kipya kimeenea kwa kasi miongoni mwa wanafunzi mjini Pretoria.