Morogoro. Kutokana na kuwapo kwa muingiliano mkubwa wa watu wakati wa ujenzi wa reli ya kisasa (Standard Gauge) eneo la Ngerengere, upimaji na elimu ya virusi vya Ukimwi inatarajiwa kutolewa kwa wakazi na wafanyakazi wa mradi huo.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro, Sudi Mpili alisema elimu na upimaji wa VVU itatolewa kwa wananchi wanaoishi na kufanya shughuli zao jirani na kambi hiyo wakiwamo wanafunzi wa shule za msingi na sekondari ili kuepuka maambukizi mapya.
“Kijiji hiki kimekuwa na muingiliano wa watu wanaokwenda kufanya kazi kwenye mradi huo na wengine kutafuta fursa za kibiashara,” alisema Mpili.
Diwani wa Ngerengere, Kibena Kingo alimuomba mkurugenzi huyo kutoa pia elimu ya afya ya uzazi na uzazi wa mpango. (Hamida Shariff)