Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dk Dorothy Gwajima ametaja vinasaba, ukatili, na mtazamo hasi juu ya changamoto za maisha kuwa sababu zinazopelekea ugonjwa wa afya ya akili.
Amezitaja sababu hizo leo akiwa bungeni Dodoma wakati akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa viti maalumu CCM, Lucy Mayenga lililolenga kujua iwapo serikali ipo tayari kupunguza muda wa kuthibitisha wagonjwa wa akili walioko kwenye magereza na mahabusu mbalimbali nchini.
Akifafanua sababu za kibaiolojia, amesema mtu anaweza kuwa anaishi na vinasaba hivyo lakini asifikie hatua ya kupata ugonjwa huo. Pia amesema mazingira ya jamii anayoishi au mazingira yake binafsi yanaweza kumuandaa kupata au kutokupata ugonjwa huo.
Ametolea mfano wa matumizi ya vilevi kupita kiasi kwa mtu mwenye vinasaba, kama mazingira yanayoweza kuchochea kupata ugonjwa huo.