Jumuiya inayowaunganisha pamoja watanzania waliopo katika sekta ya afya nchini Uingereza (Tanzania – UK Healthcare Diaspora Association-TUHEDA) imetoa vifaa tiba vyenye thamani ya Shilingi milioni 100 kwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula amesema hayo bungeni mjini Dodoma alipokuwa akiwasilisha bajeti ya makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka wa fedha 20222/2023.
Akisoma hotuba ya bajeti ya wizara hiyo, Balozi Mulamula amesema, TUHEDA imekuwa chachu ya kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Uingereza, ambapo kwa sasa majadiliano yanaendelea kuhusu kusainiwa kwa Hati ya Makubaliano baina ya nchi hizi mbili yatakayoiwezesha Tanzania kunufaika na ubadilishanaji wa ujuzi, upatikanaji wa vifaa tiba na mafunzo kwa wauguzi na madaktari.
Aidha, Mulamula amesema Diaspora wamewekeza kiasi cha Shilingi bilioni 3.9 katika mfuko wa UTT AMIS na kununua nyumba zenye thamani ya Shilingi bilioni 2.3 za Shirika la Nyumba la Taifa na mradi wa Hamidu City Park uliopo Kigamboni, Dar es Salaam.
Amesema mchango wa Diaspora umeendelea kuongezeka ambapo kwa mujibu wa takwimu za Benki Kuu ya Tanzania (BoT) fedha zilizotumwa na Diaspora nchini (remittances) ziliongezeka kutoka Dola za Marekani takribani milioni 400 mwaka 2020 hadi kufikia Dola za Marekani milioni 569.3 mwaka 2021.
Waziri Mulamula ameliambia Bunge kuwa mafanikio hayo yametokana na wizara yake kuendelea kuhamasisha Diaspora kuchangia maendeleo nchini.