Dodoma. Serikali ya Tanzania imetoa tahadhari kwa wakazi waishio maeneo yenye maambukizi ya homa ya dengue kujenga tabia ya kuvaa nguo ndefu ili kupambana na ugonjwa huo kwani mbu waenezao ugonjwa huo huuma mchana.
Mbu wa dengue hujulikana kwa majina ya Aedes Egypti, Aedes Albokictus na Aedes Africans.
Ushauri huo umetolewa na Mganga Mkuu wa Serikali, Profesa Mohammed Bakari Kambi wakati akitoa taarifa ya hali ya ugonjwa huo kwa sasa katika mikoa ya Dar es Salaam na Tanga.
“Wananchi waendelee kuchukua hatua za kujikinga ili kuepuka kuumwa na mbu kwa kuvaa nguo ndefu, kutumia vyandarua vyenye viuatilifu, kutumia dawa za kufukuza mbu na kuweka nyavu kwenye madirisha na milango ya nyumba za kuishi ili kukabiliana na ugonjwa huu,” amesema Profesa Kambi.
Usilolijua
Mbu anayeambukiza homa ya dengue, Aedes Egypti hawezi kubeba vimelea vya malaria wala yule anayeambukiza malaria hawezi kuambukiza dengue kutokana na maumbile yao.
Habari zinazohusiana na hii
Fiziolojia ya mwili wa mbu haiwezi kuruhusu Aedes kubeba virusi vya mbu mwingine na hiyo ndiyo sababu mbu hawezi kuambukiza virusi vya ukimwi.
Dengue imewahi kuripotiwa katika miaka ya 2010, 2013 na 2014 na watu wengi wanaopata ugonjwa huo hawaumwi sana na dalili zake ni kama za malaria. Wachache wanaweza kuwa na hali mbaya zaidi kama vile kutoka damu na kupata shinikizo la chini la damu.