SERIKALI imeweka wazi aina nne ya chanjo zitakazotolewa nchini dhidi ya ugonjwa wa corona na utaratibu wa kuzipata.
Chanjo zilizopewa kipaumbele kutumika nchini kwa mujibu wa mwongozo Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ni BioNTech/Pfizer BNT162b2, Moderna mRNA 1273, Novavax NVX-CoV2373 na Johnson & Johnson (Janssen) Ad26.
Mganga Mkuu wa Serikali, Dk Aifello Sichalwe, amesema mwongozo wa serikali umeanisha kila kitu wazi ikiwemo chanjo hiyo kuwa ni ya hiari.
Kwa mujibu wa Mwongozo wa Matumizi ya Chanjo ya Covid 19, ulitolewa mwezi huu kipengele cha 55, chanjo hizo ni za hiari na kabla ya mtu kuzipata atasaini fomu maalumu.
Aidha, alisema mwongozo huo umeendana na matakwa yaliyoainishwa na Shirika la Afya Duniani (WHO) ikiwemo suala la uhiari wa matumizi ya chanjo hizo.
Kauli hiyo imekuja ikiwa ni siku moja baada ya Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kuitaka serikali itoe chanjo ya Corona kwa lazima kwa kila mtu, kauli ambayo inapingana na mwongozo huo wa WHO.