Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Chanjo ya Corona kuanza kutolewa Jumanne nchni kote

B8b87843770b9f54f8fb6ec34c083c9b Chanjo ya Corona kuanza kutolewa Jumanne nchni kote

Fri, 30 Jul 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

WANANCHI katika mikoa yote nchini wataanza kupewa chanjo ya Covid-19 Jumanne ijayo kwa kuanza na makundi matatu ya kipaumbele katika vituo 550 vilivyoandaliwa nchi nzima.

Makundi hayo ambayo watapewa chanjo kwa hiari ni, watumishi wa sekta ya afya, watu wazima kuanzia umri wa miaka 50 na kuendelea pamoja na watu wenye magonjwa sugu kama vile kisukari, shinikizo la damu na saratani.

Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Profesa Abel Makubi alitoa taarifa hiyo jana alipozindua usambazaji wa chanjo hiyo katika Bohari Kuu ya Dawa (MSD) Dar es Salaam mapema leo

Alisema vituo hivyo 550 ni hospitali za umma na binafsi, vitatumika kutoa chanjo hiyo. Usambazaji wa chanjo utakamilika keshokutwa na mikoa yenye kiwango kikubwa cha maambukizi ndiyo itapokea dozi nyingi zaidi.

"Chanjo hizi ni bora na salama. Zimefanyiwa uchunguzi na Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba ( TMDA), Mkemia Mkuu wa Serikali, Maabara Kuu ya Taifa na mamlaka zingine, hivyo wananchi wasiwe na hofu," alisema Profesa Makubi.

Aliwataka Waganga Wakuu wa Mikoa na Mamlaka nyingine za serikali kuhakikisha wananchi wanapewa chanjo hizo bure na kwa hiari wakiwa na kitambulisho ama cha mpiga kura, NIDA, leseni ya udereva au kitambulisho cha kazi kuisadia serikali kutunza kumbukumbu.

Akizungumzia mzigo mwingine wa chanjo unaotarajiwa kuingia nchini kwa ajili ya wananchi wote wanaotaka kuchanjwa, alisema wananchi wanaweza kujisajili kuanzia Jumatatu kupitia tovuti ya chanjocovid.moh.go.tz na atajaza fomu ya hiari na kuchagua siku anayotaka kuchanjwa.

"Mtu anatakiwa awe na kitambulisho chake wakati wa kujaza fomu mtandaoni au wanaweza kujisajili kwenye vituo vya afya.Kila anayechanjwa anasajiliwa na kuingizwa kwenye mfumo wa kinga na atapewa cheti ambacho siyo rahisi kukinakili," alisema Profesa Makubi.

Pia aliwataka waliokwisha chanjwa kuendelea kujikinga kwa kuwa chanjo huchukua kati ya siku 14 hadi mwezi mmoja kujenga kinga mwilini.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa MSD, Benjamin Hubila, alisema dozi 3,400 za chanjo hiyo zilitumika siku Rais Samia Suluhu Hassan alipozizindua Ikulu Dar es Salaam.

Hubila alisema kwa kuwa chanjo hizo zinapaswa kutunzwa kwenye eneo lenye nyuzijoto kati ya 2-8, wana magari ya kutosha yenye kiwango hicho cha ubaridi kwa ajili ya kuzisambaza mikoani.

Mkurugenzi wa Ugavi wa MSD, Billy Singano, alisema dozi zaidi ya milioni moja za chanjo hiyo zitasambazwa kwenye mikoa yote 26 ya Tanzania Bara.

Chanzo: www.habarileo.co.tz