Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amesema kuanzia Julai mosi mwaka huu, chanjo ya Saratani ya Mlango wa Kizazi (HPV), itatolewa dozi moja badala ya mbili baada ya utafiti kubaini dozi moja inafanikiwa.
Akizungumza katika Kongamano la 31 la Kisayansi leo jijini Dar es Salaam, Waziri Ummy amesema NIMR imeweza kufanya tafiti ambazo zimekuwa msaada kwa Watanzania, ikiwemo hiyo ya chanjo ya HPV na bima ya afya kwa wote.
“Imekuwa ni taasisi muhimu katika kufanya maamuzi ya kisera kufuatia tafiti mbalimbali, mfano moja ya Tafiti waliyofanya na kukamilisha mwaka huu ni juhudi chanjo ya kuzuia saratani ya mlango wa kizazi, ambayo wanapewa wasichana wa umri wa miaka 14,” amesema.
Ummy ameeleza kuwa chanjo hiyo dozi ya kwanza wanapata watoto wengi huku ya pili ikisuasua.
“Wanakuja asilimia 70 na dozi ya pili kila watoto saba Kati ya 10 wanarudi wanne, tulikuwa na wasiwasi kama dozi moja itatosha, wamefanya utafiti na wakaja na matokea 2019 mpaka 2021 wametuambia dozi moja imeweza kuwakinga,”amesema Ummy.
“Niwaambie wazazi chanjo hii ni salmaa na inawakinga watoto ,ukienda Ocean Road katika 100 angala 26 ni wagonjwa wa saratani ya mlango wa kizazi,”amesisitiza Ummy.