UTOAJI chanjo ya virusi vya corona katika jiji la Dar es Salaam utafanyika katika maeneo ya wazi na kutumia utaratibu wa kuweka kambi siku za mwisho wa wiki kama ilivyokuwa katika Uwanja wa Uhuru Jumapili na juzi.
Mganga Mkuu Mkoa wa Dar es Salaam, Dk Rashid Mfaume alisema hayo jana alipokuwa akizungumza na HabariLEO.
Alisema, chanjo hiyo katika jiji la Dar es Salaam itakuwa endelevu na kila mkuu wa wilaya atapaswa kuandaa sehemu ambazo wananchi watafika kirahisi tofauti na vituo 51 vya chanjo vilivyotengwa awali.
"Kazi hii itafanyika kwa namna mbili, kwenye maeneo ya wazi kama vituo vya mabasi, vituo vya mwendo kasi, pantoni na masoko, namna nyingine ni maeneo ya wazi katika viwanja vya michezo kama ilivyofanyika Uwanja wa Uhuru," alisema.
Dk Mfaume alisema, maeneo ya wazi ni kwa ajili ya watu wanaofanya biashara kila siku pia kuwalenga wananchi wasioweza kufika katika vituo 51 vilivyotengwa kwa ajili hiyo.
Alisema, utoaji elimu ya chanjo utaendelea kwa sababu wananchi wanaonesha jitihada kujilinda na covid-19, ikiwamo taasisi kuzingatia kuweka maji tiririka ya kunawa na kuongezeka kwa idadi ya wananchi wanaovaa barakoa.
"Utoaji wa elimu hii hauna mwisho kwa sababu elimu inasaidia kubadilisha tabia za watu, hivyo elimu itaendelea kutolewa kila mahali," alisema Dk Mfaume.