KATIKA kukabiliana na magonjwa yasiyo ya kuambukiza kwa watu wenye umri mkubwa, Asasi isiyo ya Kiserikali ya Wakala wa Kuhamasisha Maendeleo mkoa wa Pwani (DPA) imeanza kutoa elimu ya kulima bustani za mbogamboga kama sehemu ya mazoezi kukabilina na magonjwa hayo.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi mjini Kibaha mkurugenzi wa (DPA), Rachel Jacob alisema kuwa wanafanya mradi wa kuhamasisha watu hao kuwa na bustani ili wafanye kilimo cha bustani.
"Endapo watajishughulisha itawasaidia na kuwa kama sehemu ya mazoezi wakati wanalima bustani zao mbali ya mazoezi pia watapata lishe kupitia bustani zao ambazo ni za mbogamboga,"alisema Jacob.
Alisema kuwa watu wenye umri mkubwa endapo hawatafanya mazoezi watakuwa kwenye hatari ya kupata magonjwa yasiyoambukiza .
"Kwa kuwa wao hawana shughuli za kufanya tunawapa elimu ya kuanzisha bustani za mbogamboga ili iwe sehemu ya kufanya mwili kuwa imara kwani mazoezi ni tiba hivyo tunawashauri walime bustani,"alisema Jacob.