ZAIDI ya Sh bilioni 10 zitatumika katika upanuzi wa Hospitali Teule ya Makiungu, wilayani Ikungi.
Kaimu Mganga Mfawidhi wa hospitali hiyo, Padri Stephen Samanii akisoma taarifa ya hospitali hiyo inayomilikiwa na wamisionari tangu ilipojengwa
Novemba, 1954, kwa Mkuu wa Mkoa wa Singida, Dk Binilith Mahenge, alisema hatua hiyo inalenga kuboresha huduma za afya zitolewazo hospitalini hapo na kutatua baadhi ya changamoto zinazoikabili.
“Upanuzi wa hospitali hii utahusu kujenga majengo mapya yanayokusudiwa kutoa huduma bora. Ujenzi huo hautakuwa na majengo tu bali ni pamoja na ku-
weka mashine na vifaa tiba mbalimbali vinavyotakiwa kutoa huduma,” alisema.
Alitaja baadhi ya majengo hayo kuwa ni huduma ya wagonjwa wa nje (OPD), huduma ya wagonjwa wa ndani (IPD) lenye wodi nane zenye uwezo wa vitanda 350, huduma za kiuchunguzi likiwemo la MRI, jengo la upasuaji lenye vyumba sita na vifaa vyake, mfumo mkubwa wa
uzalishaji oksijeni, jengo la kisasa la kuhifadhia maiti, jengo la kufulia, nyumba za watumishi na za watunzaji wagonjwa.
Akizungumza baada ya kusikiliza taarifa hiyo, Dk Mahenge alisema serikali ipo tayari kusaidia kutatua changamoto zinazokwamisha kufikia malengo ya hospitali hiyo kwani mradi huo ni muhimu kwa wananchi.