Morogoro. Taasisi ya Afya ya Ifakara, (IhI) imefanya utafiti na kutengeneza dawa za kufubaza Virusi vya Ukimwi (ARV) kwa watoto zilizo kwenye mfumo wa chengachenga.
Utengenezaji wa ARV za watoto katika mfumo wa chengachenga, umefanyika baada ya zile za awali za mfumo wa vidonge, kuwa na changamoto kwa watoto hasa wakati wa kumeza kutokana na ukubwa na uchungu wake.
Akizungumza na Mwananchi leo Septemba 11, Ofisa Utafiti wa IHI Ezekiel Luoga amesema Ifakara ilifanya utafiti wa kubaini mapokeo ya dawa za ARV’s zilizotengenezwa kwa mfumo wa chengachenga ambazo zitakuwa rahisi kutumiwa na watoto wenye maambukizi ya VVU.
Amesema kuwa utafiti huo wa miaka miwili ulikamilika Mei mwaka huu na ulilenga kuwapa dawa hizo watoto 85 wa wilaya za Kilombero hata hivyo mpaka utafiti huo unakamilika watoto 74 ndio walioweza kupewa dawa hizo.
“Dawa hiyo imetengenezwa nchini India na imekuwa ikitumika kwenye chakula ambapo matokeo ya utafiti yanaonesha watoto wameikubali bila ya athari zozote za kiafya,” amesema Dk Luoga
Amesema utafiti huo ulifanywa katika hospitali ya Amana jijini Dar es Salaamu pamoja na nchi za Kenya na Uganda.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Taasisi ya IhI, Honarat Masanja amesema kuwa ARV’s wanazopewa watoto ni zile zile isipokuwa zimebadilishwa mfumo kutoka kwenye vidonge na maji na sasa zipo kwenye mfumo wa chengachenga.
“Kabla ya dawa hizo hazijawekwa kwenye mfumo wa chenga chenga mzazi au mlezi alilazimika kuloweka vidonge kwenye kijiko cha maji na hivyo kupoteza ubora wake na hata ile ya maji ilikuwa na ladha chungu ambayo ilikuwa sio rafiki kwa watoto,” amesema