Serengeti. Watu 11 wakiwamo viongozi wa wazee wa mila wa koo ya Inchage wilayani Serengeti mkoani Mara wanashikiliwa na polisi wakituhumiwa kwa ukeketaji.
Jeshi la Polisi na viongozi wa mradi wa Tokomeza ukeketaji Serengeti wamethibitisha kukamatwa kwa watu hao leo.
Ofisa mradi wa Tokomeza ukeketaji Serengeti, William Mtwazi amesema wengine waliokamatwa ni wazazi na baadhi ya watoto waliokeketwa.
"Baada ya shule kufungwa baadhi ya wazazi kwa kushirikiana na wazee wa mila wakaanza kuwakeketa watoto porini na wengine nyumbani," alisema.
Septemba 12 Mkuu wa Wilaya ya Serengeti, Nurdin Babu katika kikao cha wazee wa mila alisema watakaokaidi maagizo ya Serikali na kuendelea na ukeketaji watakamatwa.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara, Juma Ndaki alipotafutwa kuzungumzia tukio hilo hakupatikana simu yake ya kiganjani ilikuwa ikiita bila majibu.
MWISHO