MIONGONI mwa mambo ambayo kila siku watanzania tumekuwa tukishuhudia Mamlaka za uteuzi, iwe Rais, Waziri Mkuu au Waziri wakitengua teuzi mbalimbali kutokana na uwajibikaji mbovu wa wateuliwa hao.
Ukiangalia kwa makini hali hiyo inasababishwa na wakati mwingine utendaji wa mazoea na kutojiongeza.
Kimsingi hatua hiyo ambayo hufanywa na viongozi wa juu wa serikali, asilimia kubwa hutokana na hatua ya viongozi hao kutoridhishwa na utendaji kazi wa watu hali inayosababisha kusuasua na pengine kukwama kabisa kwa jambo fulani katika taasisi, idara au sehemu husika.
Si kwa hilo tu, tumeshuhudia hatua za namna hiyo zikichukuliwa kwa baadhi ya viongozi hao kwa kushindwa kusimamia ipasavyo majukumu waliyopewa na hivyo kusababisha taharuki na mambo mengine mengi.
Hivi karibuni tumeshuhudia viongozi mbalimbali wakiwemo aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Albert Chalamila, aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Morogoro
Bakari Msulwa pamoja na aliyekuwa Mkurugenzi wa wilaya hiyo Sheila Lukuba kutokana na sababu mbalimbali.
Nimeandika mawazo yangu haya siyo kwa nia kutaka kuwanyooshea vidole viongozi hao na wote waliokutwa na mikasa ya aina hiyo, bali kusudi langu kubwa ni kuwakumbusha wale wote walioaminiwa katika nafasi mbalimbali kutumia vizuri madaraka yao.
Nadhani ifike mahali sasa kila aliyepewa dhamana kuona kuwa dhamana hiyo ni kubwa hivyo anapaswa kuhakikisha anafanya kila linalowezekana kwa kujitoa ili kutimiza malengo aliyopewa.