Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

Watanzania tunalo ‘deni la kumlipa’ JPM

D5368fb720fff17296e081732564a51d.jpeg Watanzania tunalo ‘deni la kumlipa’ JPM

Sun, 28 Mar 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

JUZI Watanzania tumemzika Rais wa Awamu Tano wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Hayati John Magufuli kijijini kwake Chato baada ya kufariki dunia Machi 17, mwaka huu.

Wakati tunaendelea kumlilia, tukumbuke kuwa Watanzania tunalo deni la kumlipa ‘JPM’ na hili ni hasa kumpa ushirikiano wa dhati,

Rais wa sasa, Samia Suluhu Hassan ili aendeleze gurudumu la maendeleo ya Tanzania akiendeleza safari aliyoiacha Magufuli, kudumisha amani, upendo na mshikamano, kufanya kazi kwa juhudi na maarifa na kuwa waaminifu kwa serikali ikiwa ni pamoja na kulipa kodi na kuendeleza uaminifu, nidhamu na uadilifu kwa taifa, ni mambo yatakayotufanya tuseme tunamlipa JPM deni la shukrani

Kifo cha Magufuli si tu kimegusa Watanzania, bali Afrika na ulimwengu mzima umesikitika kumpoteza shujaa kiongozi huyu asiyeyumbishwa kwa lolote mradi tu, analopigania lina maslahi kwa taifa.

Magufuli ameliliwa hata na mataifa mengine, kwa kuwa mengi yaliunga mkono mipango yake kuijenga nchi kiuchumi akitumia fedha za ndani zilizotokana na makusanyo ya kodi pamoja na rasilimali mbalimbali za nchi.

Itakumbukwa katika uhai na uongozi wake, Magufuli alisisitiza ulipaji kodi kwa dhana kuwa, kodi ndiyo chanzo kikuu cha maendeleo ya kila taifa na hivyo kujiepusha na utegemezi wa fedha za wahisani kwa ajili ya maendeleo ya nchi.

Ununuzi wa ndege ‘nyingi’ kwa malipo taslimu, ujenzi wa miundombinu ikiwemo ya barabara, reli ya kisasa (SGR), madaraja, hospitali, shule, Mradi wa Bwawa la Kufua Umeme la Nyerere na mengine mengi, ni miongoni mwa matunda ya ukusanyaji kodi za wananchi hali iliyowafanya wahamasike zaidi kuchangia maendeleo kwa kuwa wanayaona.

Ingawa Watanzania wanalia, vilio vyao vinapewa tumaini jema kwa kuapishwa kwa Samia Suluhu kuwa Rais wa Tanzania kwa mujibu wa Katiba.

Kuapishwa kwa Samia Machi 19, 2021 kuwa Rais wa Tanzania, ni faraja na tumaini kwa Watanzania kwani amefanya kazi pamoja naye kwa zaidi ya miaka mitano hivyo, anayajua mengi na njia sahihi za kuifikisha nchi katika kilele cha malengo na mafanikio.

Baada ya kifo cha Magufuli, Rais Samia amesema hakuna kitakachoharibika na kaulimbiu ya ‘Hapa kazi Tu’ ipo palepale maana yupo imara na tayari kuendelea na mapambano kuijenga nchi huku akisisitiza mshikamano na uzalendo nchini.

Watanzania wana imani kwa Samia wakisema chini ya uongozi wake, Tanzania itakuwa imara na ataendeleza aliyoyaacha mtangulizi wake.

Kimsingi, tunayo mengi ya kufanya kumuenzi Magufuli hasa kwa kumtanguliza Mungu, kudumisha amani na mshikamano na kufanya kazi kwa juhudi.

Ndiyo maana ninasema: “Watanzania tunalo ‘deni la kumlipa’ JPM.

Columnist: www.habarileo.co.tz