Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

Wanaume kuzungumzia unyanyaswaji ni haki yenu

3420afa24fbb706434f394f4898d745c Wanaume kuzungumzia unyanyaswaji ni haki yenu

Mon, 30 Nov 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

PAMOJA na matukio mengi ya unyanyasaji kuwahusu wanawake na watoto wanaofanyiwa na wanaume, kuna baadhi ya taarifa kwamba hata wanaume wengine nao unyanyaswa na wanawake lakini hawajitokezi hadharani kusema.

Mara nyingi linapojadiliwa suala la unyanyaswaji wa kijinsia imekuwa ni kawaida kusikia taarifa za ukatili unaowakuta wanawake na watoto na hii ni kutokana na asilimia kubwa ya kundi hilo kutokuwa na uwezo wa kukabiliana na manyanyaso hayo ambayo hutendwa na wanaume.

Lakini pia wapo wanaume ambao wamekuwa wakikumbana na matukio ya ukatili kutoka kwa wenza wao, hivyo licha ya uhalisia kuonesha kuwa wanawake ndio waathirika wakubwa lakini na wapo wanaume ambao wamekuwa wakinyanyaswa na wenza wao.

Binafsi ninapenda kutumia wasaha huu kuwashauri wanajamii kwa ujumla kuvunja ukimya na kutoka nje kuzungumzia namna bora ya kukabiliana na unyanyaswaji wa kijinsia.

Napenda na kuanza na baadhi ya wanaume ambapo kuna mtazamo kuwa iwapo mwanaume akijitokeza kuzungumzia unyanyaswaji ataonekana dhaifu.

Haya ni kati ya mambo yanayokwamisha idadi kubwa ya wanaume kushindwa kujitokeza kwenye madawati ya kijinsia kupeleka malalamiko yao kuhusiana na unyanyaswaji wanaofanyiwa na wenza wao hivyo kujikuta wakiendelea kunyanyasika na kuishia kuzidi kuathiriwa kisaikolojia.

Kati ya wanaojitokeza kulalamikia unyanyaswaji katika madawati ya jinsia vituo vya Polis wanawake wanaweza kujitoeza 20 na mwanaume mmoja.

Ni muda wa kuondokana na dhana kuwa mwanaume anapaswa kuvumilia, mwanaume ni shupavu au mwanaume hawezi kudharirishwa na mwanamke, na badala yake kujitokeza kuomba msaada kwa kuwa kwanza ni hatari zaidi kwa mtu kukaa kimya dhidi ya kero hizo kwa kuwa anaweza kulipa kisasi kwa kufanya mambo mabaya zaid.

Kati ya mambo ambayo yamekuwa ni ukatili dhidi ya wanaume ni pamoja na kudhauriwa na mwenza kutokana na changamoto ya kipato, kunyimwa haki ya unyumba na kuona watoto na mengine mengi.

Ifahamike kuwa madawati ya jinsia yenye jukumu na kusikiliza manyanyaso ya kijinsia yaliyopo kwenye vituo vya Polisi ni kwa ajili ya jinsia zote yani wanawake na wanaume, hivyo kila mtu ana haki ya kuwasilisha kero zake.

Kwa kuwa kipindi hiki cha maadhimisho ya siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia wadau mbalimbali wanafanya kampeni za kuelimisha masuala hayo ikiwa pamoja na kusikiliza malalamiko, ni vema jamii yote kwa ujumla kushiriki kwa kujitokeza kupinga ukatili wa kijinsia pamoja na kuzungumzia suala hilo kuanzia ngazi za familia.

Tanzania imeungana na nchi nyingine duniani kufanya maadhimisho hayo ya kupinga ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake na watoto huku kauli mbiu ikiwa ni “Mabadiliko Yanaanza na Mimi.”

Maadhimisho hayo yaliyoanza Novemba 25 yanaendelea sehemu mbalimbali nchini ambapo mijadala inaendelea katika kila kona ya nchi na tamati yake kufikiwa Desemba 11, tukio litakaloendana na utolewaji wa tuzo maalum ya heshima kwa vinara dhidi wa mapambano dhidi ya unyanyaswaji wa kijinsia.

Kwa mujibu wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Haki za Watoto (Unicef), wanawake milioni 750 wameolewa kabla ya umri wao huku wasichana milioni 120 wamefanyishwa ngono bila ya ridhaa yao.

Kwa hapa nchini kwa mujibu wa ripoti ya Ofisi ya Takwimu ya Taifa (NBS) ya mwaka 2015-16, asilimia 40 ya wanawake wenye umri kati ya miaka 15 hadi 46 wamefanyiwa ukatili wa kijinsia, huku asilimia 20 kati ya umri huo wamefanyishwa ngono bila ya ridhaa yao.

Columnist: habarileo.co.tz