Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

Wabunge rudini majimboni

16a4c0c6d7d2cdc099b9fd98d9e942d5.jpeg Wabunge rudini majimboni

Mon, 19 Jul 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

TANGU kumalizika kwa Bunge la bajeti mwanzoni mwa mwezi huu, wapo baadhi ya wabunge wamerejea katika majimbo yao kwa ajili ya kukutana na wapiga kura wao ili kusikiliza au kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili.

Huu ni wakati muafaka kwa wao kufanya hivyo kwa kuwa ndiyo muda ambao wana nafasi ya kutosha baada ya shughuli za vikao vya Bunge kuharishwa kusubiri Bunge lijalo panapo maajaaliwa ya Mwenyezi Mungu.

Ukiachlia mbali mawaziri ambao pia ni wabunge, imani yangu ni kuwa wabunge wengine wote kwa sasa watakuwa ndani ya maeneo ya majimbo yao kuhakikisha wanazifanyiakazi changamoto za wananchi.

Nasema hivi kwa sababu, kwa kipindi hiki ambacho vikao vya Bunge vimesimama hakuna sababu nyingine yoyote ya Mbunge kutoonekana jimboni kwake kwa kigezo cha kubanwa na majukumu mengine isipokuwa mawaziri ambao wapo kutekeleza majukumu ya serikali.

Niwapongeze wabunge wote ambao wametambua wajibu wao na kuamua kurejea majimboni kwa ajili ya kukutana na kuzungumza na wapiga kura wao ili kufahamu changamoto za hapa na pale kisha kuzifanyia kazi.

Imezooleka kuwa, baadhi ya wabunge ambao siyo nia yangu kuwataja hapa, badala ya muda huu kurejea kwa wapiga kura, wao wapo mijini na maeneo mengine tofauti wakila 'bata' wakisahau kipindi cha kampeni waliyokuwa wakihaha kuomba ridhaa hiyo kutoka kwa wananchi.

Narudia tena, wawakilishi hao wapo na wanafahamika vizuri, kikubwa ni wananchi wenyewe kujitathimini kama wanapenda kuendelea kuwa na mla bata au kiongozi wa kushirikiana nao jimboni wakati wote.

Si ajabu kusikia kuwa wapo baadhi ya wabunge ambao tangu wamechaguliwa kushika nafasi hiyo hawajaonekana tena majimboni baada ya walichokuwa wakikitafuta kukipata wakiamini kuwa baadae watakwenda tena kuwalaghai wananchi na kuchaguliwa tena.

Hivi karibuni Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi, Daniel Chongolo alitoa msisitizo katika suala hilo kwa kuwataka wabunge wa chama hicho kurudi katika majimbo yao na kusikiliza kero za wananchi akisema kuwa huo ndiyo utaratibu na msimamo wa chama hicho.

Kauli hii ya kiongozi wa juu wa CCM ni wazi ameitoa akitambua wazi kuwa wapo baadhi ya wabunge wenye tabia hiyo ya 'kuwakacha' wananchi wao huku baadhi yao wakijenga majumba mjini baada ya 'kulamba' ubunge na kusahau kabisa maisha ya majimboni walikopata ubunge.

Mwenye macho haambiwi ona, na mwenye masikio haambiwi tazama, watakaokwenda majimboni wananchi watawaona na kuwasikia, hivyo ni jukumu lenu kusuka au kunyoa, lakini niwatahadharishe Watanzania wa siku hizi ni waelewa sana wakisaidiwa na ukuaji wa teknolojia ya mtandao, hicho mtakaowatekeleza mkae chonjo maana uchaguzi mwingine haupo mbali.

Columnist: www.habarileo.co.tz