Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

Wabunge Viti Maalumu Chadema mmewatendea haki Watanzania

A907f57573c49fa6044ce81c42db49f6.png Wabunge Viti Maalumu Chadema mmewatendea haki Watanzania

Thu, 26 Nov 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

NIANZE wazo langu kwa kusema: “Katika hili, wabunge 19 wa viti maalumu Chadema, mmeona mbali na mmewatendea haki wapiga kura wa Tanzania na kimsingi, sasa mmeonesha uzalendo.”

Ikumbukwe kuwa, baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 28, 2020 wa Rais, Wabunge na Madiwani, wabunge wote waliochaguliwa na hata waliotokana na viti maalumu, waliapishwa bungeni isipokuwa tu, wabunge 19 wa viti maalumu kutoka Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).

Hali hii ilitokana na baadhi ya viongozi wakuu wa Chadema, kuwazuia wanachama wake ama waliochaguliwa, au kuteuliwa kwenda bungeni kwa madai kuwa, chama hicho hakitambui uamuzi walioufanya Watanzania katika sanduku la kura. Ajabu!

Katika hali inayoonesha kuwa wapo watu wenye mawazo ya kijamaa katika nchi za kibebapri na kadhalika wenye mawazo ya kibepari katika nchi za kijamaa, baadhi ya viongozi wa Chadema wamechambua kutoka matandu hadi makoko ya ukweli na kubaini kuwa, mgomo huo hauna tija kwa wanachama wa Chadema na chama chao, wapiga kura wao na taifa kwa jumla.

Wanachama hao na viongozi wa Chadema wameuvaa uzalendo na Utanzania halisi na kujitokeza kuonesha shukrani zao kwa Watanzania waliokipigia kura chama chao hadi kupata sifa ya kupata nafasi 19 za viti maalumu bungeni.

Ninasema ninawapongeza kwani kitendo chao kwenda mbele ya Spika wa Bunge, Job Ndugai na kuapa kuwa wabunge kwa mujibu wa taratibu na kanuni za Bunge, kimeonesha kuwa wanatambua lengo la bunge kuwa na viti maalumu kwamba ni kuongeza uwiano na fursa za uwakilishi wa wanawake katika siasa na uongozi hali inayohitimishwa na uwakilishi unaolenga usawa wa kijinsia katika vyombo vya maamuzi.

Ninawapongeza wabunge wa viti maalumu Chadema kwani wametafakari na kuukabali ukweli kuwa, mbunge bora kwa jamii ni yule anayetambua kuwa, kwanza, anawajibika kwa taifa lake, kwa jimbo lake, kwa chama chake na mwisho, kwake na familia yake.

Ikumbukwe kuwa, wabunge wa viti maalumu na wabunge wa kuteuliwa na rais, ni wabunge wa taifa zima hivyo, wanao wajibu wa kusikiliza sauti za wananchi kuliko hasa sauti ya chama maana chama ni kwa ajili ya watu na si watu kwa ajili ya chama.

Kitendo cha wabunge hao kujitoa kuwatumikia Watanzania, huku baadhi ya viongozi wakuu wa chama wakitishia kuwachukulia hatua kwa kuwaita katika vikao vya chama, kinaonesha kuwa wameamua waziwazi kuunga mkono juhudi za watetezi wa haki za binadamu na usawa wa kijinsia.

Hiivi karibuni wakati akizungumza katika mkutano wa kwanza wa bunge la 12, Spika wa Bunge, Job Ndugai alisema kwa mshangao kuwa, kama wabunge wa viti maalumu wangekuwa ni wanaume, wote wangekuwa tayari wapo bungeni, lakini kwa vile ni wanawake, viongozi ambao wengi ni wanaume, wanawazuia.

Mfumo dume huu kimsingi, ‘unabemenda’ demokrasia katika vyama vingi vya upinzani kwa wanachama na viongozi wanawake kuamriwa kila jambo hata lisilo na maslahi kwao, kwa chama wala kwa taifa.

Ndiyo maana ninasema wabunge 19 wa viti maalumu Chadema, sasa mmewatendea haki wapiga kura na Watanzania kwa jumla kwa kujitoa kuwatumikia ama uwe wakati unaofaa, au usiofaa na ndiyo maana Spika Ndugai ameahidi kuwalinda na kuwapa ushirikiano wote.

Columnist: habarileo.co.tz