Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

WAZO LANGU: Tunataka bingwa halali Ligi Kuu

951489ad12c9523d9769ff19ad8e3851.png Tunataka bingwa halali Ligi Kuu

Sat, 26 Feb 2022 Chanzo: www.habarileo.co.tz

Mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara umeanza jana kwenye Uwanja wa Nyankumbu Geita ambapo wenyeji walitarajiwa kucheza na Namungo.

Mpaka mzunguko wa kwanza ulinamalizika, Yanga ndiyo ilikuwa ikiongoza ligi hiyo ikiwa na pointi 39 ikifuatiwa na Simba yenye pointi 31 na Azam ikishika nafasi ya tatu ikiwa na pointi 24, huku Prisons, ikishika mkia ikiwa na pointi 11.

Timu nyingine zinazoshiriki Ligi Kuu ni Mtibwa Sugar, Coastal Union, Kagera Sugar, Ruvu Shooting, Mbeya Kwanza, Mbeya City, Geita Gold, Biashara United, Polisi Tanzania, Dodoma Jiji na KMC.

Natarajia timu zinazoshiriki Ligi Kuu zilitumia muda wa mapumziko vizuri kujiandaa kwa ajili ya mzunguko wa pili.

Naamini katika kipindi hiki cha lala salama ni wakati wa timu kutazama wapi ziliteleza na kufanyia marekebisho makosa yao kabla hazijaenda nje ya mipango yao.

Nasema hivyo kwa sababu katika mzunguko huu wa pili wapenzi wa soka wanatamani kushuhudia ushindani mkubwa wa timu, tofauti na ulioonekana katika mzunguko wa kwanza, ili tupate bingwa anayestahili kweli kutuwakilisha katika mashindano ya kimataifa.

Pia, katika mzunguko huu wa pili tunatarajia kushuhudia ushindani kwa wachezaji, tunataka kuona wachezaji wakionesha vipaji vyao na kushirikiana ili kuleta mvuto kwa mashabiki wapya wa Ligi Kuu na kuendelea kuwahamasisha mashabiki wa zamani wa Ligi Kuu kujitokeza viwanjani.

Katika mzunguko huu wa pili, binafsi natarajia wachezaji wataonesha vipaji vyao na nidhamu ya juu, pia naamini Bodi ya ligi itakuwa na ratiba isiyopanguliwa mara kwa mara.

Aidha, pia naamini kasoro zilizoonekana kwenye baadhi ya viwanja zimerekebishwa, maana katika mzunguko wa kwanza makocha wengi walilalamika ubovu wa viwanja.

Ni imani yangu waamuzi katika mzunguko huu wa pili wa ligi watajitahidi kwa kiasi kikubwa kusimamia sheria 17 za soka na kama kuna upungufu basi uwe ule wa kibinadamu tu.

Ni wazi waamuzi wana kazi kubwa ya kufanya ili ligi iwe na mvuto zaidi na kazi hiyo ni kuchezesha Ligi Kuu kwa haki na kutoa uamuzi sahihi na siyo kutoa uamuzi kwa shinikizo la watu wenye nguvu au kukoseakosea kutoa uamuzi au kupokea rushwa kupindisha uamuzi.

Waamuzi wanatakiwa kuelewa kuwa uamuzi ni wito na mwamuzi anapochezesha anatakiwa kujiamini na siyo kuwa mnyonge kwani hawezi kutoa uamuzi halali kama atakuwa anatawaliwa na wachezaji uwanjani au kuogopa lawama za makocha.

Ni dhahiri kuna upungufu mwingi uliojitokeza katika mzunguko wa kwanza na mara kwa mara vyombo vya habari vimekuwa vikizungumzia hilo lakini haufanyiwi kazi. Tunatarajia mzunguko huu wa pili wa Ligi Kuu utaongozwa kwa kufuata kanuni kwa kufanya hivyo tutakuwa na ligi bora na yenye ushindani wa hali ya juu.

Columnist: www.habarileo.co.tz