Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

WAZO LANGU: Kauli ya Karia inatosha kuwa mwongozo kwa waamuzi Ligi Kuu

Waamuzi Ligi Kuu Waamuzi wa Ligi Kuu ya NBC wakiwa kwenye Semina

Sat, 19 Feb 2022 Chanzo: www.habarileo.co.tz

Waamuzi ni watu muhimu kwenye mchezo wa soka kokote kule, lakini pindi wanaposhindwa kufuata sheria za uchezeshaji huaribu kila kitu.

Kauli ya Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Wallace Karia kuhusiana na kuvurunda kwa waamuzi ilikuwa na maana nzito na kama watu waelewa wanapaswa kubadilika.

Karia amewaambia waziwazi kwamba baadhi yao siyo waaminifu na ndio wanasababisha tafrani kubwa huko mitaani kutokana na mapenzi yao kwa timu wanazozipenda na mbaya zaidi matusi anatukanwa yeye.

Waamuzi wanapaswa watafakari maneno mazito ya Karia, kwani hakuna ubishi ligi ya Tanzania imekuwa na maendeleo makubwa na mazuri miaka ya karibuni lakini lawama na kelele kuhusiana na uchezeshaji wao kutaondoa imani.

Imani itaondoka kwa wawekezaji lakini pia mashabiki ambao wanadhani kuna timu fulani ambayo imeandaliwa kuwa bingwa sasa hiyo ndio inaleta kelele kila kukicha na kupoteza maana halisi ya ligi yenye ushindani.

Hakuna ubishi waamuzi nao ni binadamu na wana haki ya kukosea ili kukamilisha ubinadamu wao, lakini isiwe kwa timu moja au mbili tena katika mechi zinazofuatana.

Waamuzi hao watambue kuvuruga kwao lawama zinamwangukia Karia na Kamati nzima ya Waamuzi ingawa wao wanahusika katika kuwapanga lakini siyo kutoa maagizo kwamba wahakikishe timu fulani inafungwa au kukataliwa bao lake.

Waamuzi wanapaswa kutambua kwamba mchezo wa soka ni burudani yenye kumfurahisha mchezaji na mtazamaji bila kujali matokeo ya mchezo lakini ikitokea yeye ametumia mamlaka yake ya uchezeshaji vibaya na kuipa bao lisilo la halali timu nyingine kuna asilimia kubwa ya amani kutoweka ua namba ya mashabiki kupungua viwanjani.

Kitu cha msingi hapa kwa Waamuzi pamoja na ubinadamu waliokuwa nao lakini wanapaswa kuhakikisha wanakuwa makini na kuzitafsiri ipasavyo sheria wanapokuwa uwanjani ili kutoa haki sawa kwa kila upande na kupunguza kelele ambazo hivi sasa zimeenea kuhusu sekta hiyo.

Mbali na hivyo lakini pia kupunguza kwao makosa kutapandisha thamani kwa ligi yetu lakini pia kutasaidia kumpata bingwa na mwakilishi bora wa Tanzania katika michuano ya kimataifa.

Kubwa zaidi kutamweka salama Rais Karia na timu yake sababu nao ni miongoni mwa wanaotajwa kuwa wanahusika katika kutoa maagizo kwa waamuzi ili kuisaidia timu fulani kupata matokeo.

Makosa kwenye mchezo wa soka yapo hata huko Ulaya ambako wana teknolojia ya VAR, bado makosa yanafanyika lakini kwa hapa kwetu yamezidi mengine hayahitaji hata VAR kuyang’amua sasa wana hitajika kujibidiisha ili kuendana na wakati tuliopo.

Waamuzi watumie kauli ya Rais wa TFF, na mafunzo waliyoyapata kwenye semina hiyo ili kuboresha viwango vyao na kuinogesha ligi yetu kwa ushindani na kutenda haki na siyo kutegemea kamati ya masaa 72 kutoa adhabu kwa matukio ambayo yalishapita na kusahaulika.

Columnist: www.habarileo.co.tz