Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

Uhuru wa siasa usiwe mtaji wa vurugu

49daa7eb74879adeeef7b16b2a73d4f3.jpeg Uhuru wa siasa usiwe mtaji wa vurugu

Wed, 11 Aug 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

TANZANIA ni miongoni mwa nchi zinazoendesha mfumo wa siasa wa kidemokrasia wa vyama vingi ulioanza nchini mwaka 1992.

Tangu hapo, Watanzania kupitia vyama mbalimbali wamekuwa wakishiriki Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani.

Sisi tunawapongeza Watanzania wote waliojitokeza kukoleza moto wa demokrasia katika mfumo huu siasa unaosendelea kustawi hadi sasa.

Kipekee tunawapongeza wote ‘wanaocheza ngoma’ ya demokrasia ya siasa katika mfumo huu kwa makini, ungwana na ustaarabu huku wakitanguliza maslahi ya Tanzania, na si maslahi yao binafsi na mabeberu ama wawe wa ndani, au nje ya nchi.

Tunasema tunawapongeza hao kwani tunajua wazi kuwa penye msafara wa mamba kenge hawakosekani hivyo, katika safari hii ya kuijenga Tanzania kiuchumi na kisiasa, wapo pia ‘mateka wa kisiasa’ waliotekwa na mabeberu hususan wa nje ya nchi, ili watumike kuchafua sura ya Tanzania kwa kuendesha siasa za vurugu.

Kipekee tunasema, Watanzania wazalendo na makini hawana budi kupuuza hila za wanasiasa uchwara wa namna hiyo wanaotumiwa na baadhi ya mataifa ya nje kutaka kuhalalisha vurugu nchini, eti kwa kujificha kwenye mwamvuli wa demokrasia ya siasa katika mfumo wa vyama vingi.

Kimsingi, hakuna demokrasia yenye tija kama watu wataitumia kuanzisha na kuchochea vurugu, badala ya kuchochea umoja, upendo, maendeleo na mshikamano wa kidugu maana siasa ni kwa ajili ya watu na si watu kwa ajili ya siasa.

Ndio maana tunaipongeza serikali kwa kuendelea kutoa uhuru wa kisiasa kwa kila mtu, lakini tunaihimiza serikali kuendelea kuhakikisha kuwa, hakuna anayetumia uhuru wa kisiasa (demokrasia) kuanzisha na kuendesha fujo nchini.

Likifanyika kosa la kuruhusu watu au kikundi cha watu kujificha katika demkorasia kufanya vurugu , litasababisha hatari ya kuwaingiza Watanzania katika upotevu wa amani.

Ndio maana tunasema: ‘Uhuru wa siasa usiwe mtaji wa vurugu.’

Columnist: www.habarileo.co.tz