Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

UBISHI WA MZEE WA KALIUA: Saido anataka kuwaibia Yanga kama 'Auba' kwa Arsenal

Saido Pic 1 Data Saido anataka kuwaibia Yanga kama 'Auba' kwa Arsenal

Thu, 3 Feb 2022 Chanzo: www.mwanaspoti.co.tz

Niliacha kila kitu na kutega sikio langu kwa makini ili nilisikie tena jibu la kocha wa Arsenal, Mikel Arteta. Mwanzoni nilidhani Arteta anatania lakini haikuwa hivyo.

Aliendelea kusisitiza kwamba yeye na Arsenal hawana mpango wa kuendelea kuishi na mshambuliaji raia wa (Gabon), Pierre Emerick Aubamayeng. Kisa? Kwanza ni utovu wa nidhamu. Pili ni kuporomoka kiwango kwa kiasi kikubwa.

Hii sababu ya pili inaweza kumtokea mchezaji yeyote. Kinachowakera zaidi Arsenal ni kwamba Aubamayeng mwenyewe hakuonyesha kujali wala kukerwa na kiwango chake kibovu. Ndiyo sababu walitaka aondoke.

Wanachosahau Arsenal ni kwamba haya maisha walimtengenezea Aubamayeng wenyewe. Mwaka mmoja na nusu uliopita Auba alikuwa katika kiwango bora cha maisha yake na mkataba wake ulikuwa unaelekea ukingoni.

Arsenal walijitutumua kumlazimisha asaini na kweli mwisho wa siku Auba alisaini mkataba mnono zaidi kuwahi kuusaini maishani mwake. Alisaini mkataba wa miaka mitatu unaompatia Pauni 350,000 kila mwisho wa wiki.

Baada ya hapo Auba hajawahi kukamata makali yake tena. Ule uwezo wake uliowahangaisha Arsenal kuharakisha kumpatia mkataba mpya uliondoka na wino aliomwaga kutia saini katika karatasi ya mwisho mkataba wake.

Nini kilitokea ghafla? Ukweli ni kwamba baada ya kupata kandarasi mpya Auba hakuwa na kitu kingine anachohitaji zaidi.

Kabla ya mkataba alijitoa kila alivyoweza ili kuwalazimisha Arsenal kumpatia mkataba wa muda mrefu. Alijua utaisha akiwa amekusanya pesa za kutosha kisha atatokomea zake huko China au Marekani kwenda kumalizia maisha yake ya soka.

Kwa lugha rahisi tunaweza kusema Arsenal walikosea kumpa Aubamayeng mkataba wa miaka mitatu akiwa na umri wa miaka 31. Licha ya hivyo bado hatuwezi kuwalaumu Arsenal. Walichofanya ni kutazama kile Auba alichokuwa anakifanya kwa wakati ule kisha wakampatia walichoona anastahili kupatiwa. Isingekuwa rahisi kutabiri kwamba Auba ataporomoka kiwango kwa kasi kutokana na ubora aliokuwa nao wakati ule.

Ni kama ambavyo ni ngumu kwa sasa kutabiri kwamba, kiungo wa Yanga, Saido Ntibazokinza anaweza kuporomoka kiwango mwaka ujao kutokana na ubora anaouonyesha kwa sasa.

Msimu ulianza vibaya kwa Saido Ntibazonkiza. Hakuwa na furaha ndani ya Yanga kwa sababu hakuwa sehemu ya kikosi cha kwanza. Mara nyingi aliachwa jukwaani au aliwekwa benchi kwa sababu ya ufinyu wa nafasi.

Aliumia Yacouba Sogne na ghafla Saido alipata nafasi. Tangu alipopata nafasi Saido hajawahi kufikiria kurudi nyuma. Amekuwa akiongezeka ubora siku baada ya siku na sasa ni mmoja wa wachezaji tegemeo ndani ya Yanga.

Mwisho wa msimu uliopita Yanga waliweka jina lake kwenye ‘red list’ kwamba lazima aondoke. Lakini ghafla idadi ya wachezaji wa kigeni iliongezeka kisha akaondoka Tuisila Kisinda na kujikuta nafasi ya Saido inapatikana. Yanga wakakubaliana wamvumilie kwa msimu mmoja mwingine. Ni msimu huu ambao mkataba wake unakatika ndani ya miezi sita ijayo.

Yanga hawakuwahi kufikiria kama siku moja watamshuhudia Saido katika ubora huu alionao sasa. Saido amepata nafasi na amerudisha swali kwao. Amewaweka katika kizungumkuti.

Je wampe mkataba mpya kutokana na wanachokiona sasa? Lakini vipi kama Saido anawaibia? Vipi kama anawaonyesha ubora huu ili wampe mkataba mpya kisha arudi kule alipokuwa? Ni maswali magumu ambayo Yanga hawajui wanayajibu vipi.

Iliwahi kutokea kwa Haruna Niyonzima pale Simba. Alitumia miaka miwili kukaa benchi au jukwaani baada ya Simba kutumia nguvu kubwa kumng’oa Yanga. Ilipofika miezi ya mwisho ya mkataba wake akawasha moto kuwaaminisha Simba kuwa amezaliwa upya.

Simba wakaanza kutafutana lakini baadaye walikuwa wajanja wakamuacha aondoke. Waligundua Niyonzima alikuwa anawadanganya. Ni kitu kama hiki kitawasumbua Yanga kwa Saido.

Lakini pia unampongeza Saido kwa kuwa mjanja katika kuiuza saini yake. Nyakati ambazo mkataba unaelekea mwisho mchezaji inabidi uzishtue klabu zingine zikutolee macho. Ni kama ambavyo Antonio Rudiger anafanya kwa sasa pale Chelsea kule England.

Kama leo Yanga wataamua kuachana na Saido hawezi kukosa klabu nne au tano ndani ya Ligi Kuu Bara zitakazopigana vikumbo kuipata saini yake.

Ni lazima atavuna pesa zingine nyingi kutokana na usajili wake. Ni akili kama hizi za kina Saido Ntibazonkiza inabidi wachezaji wetu waziige. Mchezaji unamalizaje mkataba na klabu kubwa nchini halafu klabu ndogo hazipiganii saini yako?

Columnist: www.mwanaspoti.co.tz