Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

Tuwape nafasi wateuliwa watekeleze wajibu wao

D1f32d84a415f45406ea96ec989d3852.png Tuwape nafasi wateuliwa watekeleze wajibu wao

Fri, 2 Apr 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

RAIS Samia Suluhu siku chache zilizopita alifanya mabadiliko kidogo kwenye Baraza la Mawaziri, huku pia akiwateua wabunge kadhaa ambao baadhi yao amewapa nafasi ya kuwa sehemu ya baraza hilo.

Ninampongeza Rais Samia kwa hatua hizo kwa sababu yeye ndiye dereva wetu awamu hii na ndiye anayefahamu nani anaweza kumsaidia zaidi katika eneo fulani na nani amuweke eneo jingine na hayo ni maamuzi yake ambayo tunapaswa kuyaheshimu na kazi yetu sisi ni kutoa ushirikiano kwa sababu nchi inajengwa na sisi sote.

Nasema hayo kwa sababu kumeibuka makundi ya watu na wengine mmojammoja ambao wanadhani wao ni mabingwa kwa kufanya uchambuzi wa kila jambo hata kwa safu anayopanga Rais kumsaidia.

Watu hao wanasahau kwamba, urais ni taasisi ambayo inapaswa iachwe ifanya kazi zake kwa uhuru na sisi wengine tusaidie ujenzi wa taifa hili kwa kutimiza majukumu yetu kila mmoja mahali alipo na kama kuna jambo la kushauri liwasilishwa kwa njia ipasayo badala ya kila mmoja kujifanya bingwa wa kuwachambua wateuliwa wa urais.

Tutambue kwamba hakuna aliyemkamilifu chini ya mbingu, kila mmoja ana mazuri na mabaya yake na pia utendaji kazi wetu unatofautiana kuna mwingine ni mzuri kwenye eneo Fulani na mwingine eneo jingine, hivyo tuwaache wafanye kazi katika maeneo yao waliyopangiwa kumsadia Rais kwani sote tunajenga nyumba moja ambayo ni Tanzania ili iwe mahali bora kwa kuishi kwa kila mmoja.

Katika mitandao ya kijamii baadhi ya watu wamekuwa hodari sana kuwachambua kila jambo hata wasilokuwa nalo na uelewa wa kutosha kana kwamba wao ni malaika hawana mapungufu yao.

Tusiwe na tabia ya kuhukumu mtu kwa mapungufu yake machache tu kama yapo, wakati yapo mazuri mengi yanayomuhusu.

Tuacha tabia hizo mbaya ambazo hazina tija wala hazileti faida kwa nchi yetu bali tuungane katika kulijenga taifa letu.

Tuijenge Tanzania mithili ya watu wajengao nyumba, mmoja akileta fito, mwingine alete misumari, mwingine bati, mwingine saruji, mwingine maji, mwingine kokoto, mwingine mchanga na mwingine mbao na nondo.

Kwa pamoja tutaijenga nyumba imara ambayo ni Tanzania lakini iwapo tutaanza kuwanyooshea vidole wateuliwa na kuacha kuungana kuijenga nchi hakika taifa litagawanyika na lawama zitabaki kwetu.

Tuwape nafasi wateuliwa wa Rais watekeleze wajibu wao na sisi tusiwe sehemu ya kuwakwamisha ili baadaye kuwalaumu kuwa wameshindwa, bali tuwasaidie kutimiza wajibu wao kwa sababu kazi ya maendeleo sio ya mtu mmoja bali inahitaji ushirikiano wa sisi sote.

Tujenge tabia ya siafu au nyuki wanavyofanya kazi kwa umoja hakuna anayekaa pembeni kukosoa utendaji kazi wa mwingine kila mmoja anatimiza wajibu wake na hatimaye maendeleo yanaonekana, tuache tabia ya kukosoa kila kitu hata mazuri yanayofanywa kwani kwa kufanya hivyo hatutaendelea tutakuwa taifa la kulalamika tu.

Rais Samia anahitaji msaada wangu na wako, kazi ya kuongoza nchi sio jambo dogo tusipowajibika wote nchi haitaendelea, tuache kujifanya tunajua sana kuwachambua kwa ubaya wanaoteuliwa kwani sisi sote tuko hivyo kila kila mmoja Mungu kampa karama yake, tuwatie moyo na kuwaombea ili waweze kufanya vizuri.

Lakini pia, tutambue katika kuijenga nchi yetu, baadhi yetu ama kwa kujua au kutokujua wanaweza kushawishiwa na wasioitakia mema Tanzania na kuwabadilisha mtazamo kuona kila linalofanywa na viongozi wetu ni baya na watakuwa mstari wa mbele kukosoa kila kitu, hao tuwe macho nao.

Columnist: www.habarileo.co.tz