Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

Tushirikiane na serikali kutimiza ndoto za JPM

9aa300ef6988c7562849b78f5ad75530.jpeg Tushirikiane na serikali kutimiza ndoto za JPM

Thu, 15 Apr 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

PAMOJA na kwamba siku 21 za maombolezo zimemalizika na maisha ya Watanzania yamerejea kama kawaida, pengo la kifo cha Rais wa Awamu ya Tano, Dk John Magufuli haliwezi kuzibika kwani kila mtu amejaaliwa karama zake juu ya namna ya kutekeleza majukumu yake hasa kama ni kiongozi.

Katika hotuba zake zote wakati na baada ya msiba wa Magufuli, Rais Samia Suluhu Hassan amekuwa akiwahakikishia Watanzania kuwa, serikali itahakikisha urithi wa miradi mikubwa ulioachwa na Magufuli unalindwa na kuendelezwa kwa faida ya kizazi cha sasa na cha baadae.

Samia mara zote amekuwa akieleza kuwa, ipo miradi iliyokuwa imeanza chini ya uongozi wa mtangulizi wake (Magufuli) yeye akiwa Makamu wa Rais na kuwaeleza wananchi kwamba, miradi hiyo ni urithi kwa taifa hivyo serikali itahakikisha inatekelezwa na kukamilika kwa wakati.

Aidha, juzi Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akizungumza bungeni jijini Dodoma, aliainisha mambo kadhaa yatakayotekelezwa na serikali katika mwaka wa fedha 2021/2022 kuenzi na kuendeleza jitihada, maono na juhudi za Dk Magufuli pamoja na kuhakikisha miradi yote ya kimkakati inakamilika.

Majaliwa alisema hayo wakati akitoa hotuba ya bajeti ya mwaka wa fedha 2021/22 ya ofisi yake. Alisema kati ya mambo watakayomuenzi nayo Dk Magufuli ni pamoja na ulinzi wa rasilimali za taifa, nidhamu katika matumizi ya fedha za umma, utekelezaji wa miradi ya kimkakati na lugha ya Kiswahili.

Mengine ni mapambano dhidi ya rushwa na ufisadi, kuwajali wananchi wanyonge na kudumisha umoja wa kitaifa, huku wakitekeleza kwa kasi miradi ya kimkakati ambayo inalenga kukuza uchumi, kuimarisha huduma za jamii na kuongeza fursa za ajira.

Majaliwa aliwahakikishia Watanzania kuwa, serikali itaendelea kuongeza nguvu kuendeleza na hatimaye kukamilisha miradi hiyo na pia itaimarisha huduma za jamii zikiwemo afya, elimu na maji pamoja na kuanzisha miradi mipya.

Naye Makamu wa Rais, Philip Mpango alikazia hilo siku alipoapishwa kushika madaraka hayo kwa kumuhakikishia Rais Samia, viongozi wa serikali na Watanzania wote kuwa, yale mema yaliofanywa na Dk Magufuli ambayo pia yalisimamiwa kwa karibu na Samia akiwa Makamu wa Rais, yataendelezwa.

Kauli hizi za viongozi wa juu wa serikali zinadhihirisha dhamira ya dhati ya kuipeleka Tanzania kwenye mapinduzi makubwa ya uchumi na huduma bora kwa jamii.

Hata hivyo, kufanikiwa kwa malengo haya kunategemea kwa kiasi kikubwa nguvu ya pamoja baina ya serikali na wananchi. Hili si jambo la kuisubiri serikali ifanye au ishindwe ili tupate cha kusema bali wananchi tunapaswa kushirikiana nayo kwa kutekeleza wajibu wetu kila mtu kwa sehemu yake.

Huu ni wakati kwa watendaji wa serikali kuhakikisha nchi inafikia malengo, kwa wananchi hatupaswi kuwatakatisha tamaa viongozi, kulaumu au kuponda uongozi ili kuhakikisha mema na ndoto zote njema za Dk Magufuli na watangulizi wake kwa taifa hili zinatimia.

Columnist: www.habarileo.co.tz