Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

Tuongeze juhudi zaidi kuondoa ajali barabarani

1d8722a6dfe6e615b96d110cab2f82f7 Tuongeze juhudi zaidi kuondoa ajali barabarani

Mon, 16 Nov 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

HABARI kwamba ajali za barabarani nchini zimepungua kwa asilimia 35 hadi 28 kwa mwaka, vifo navyo vikiwa vimepungua kutoka asilimia 31 hadi 19 na kwamba majeruhi nao wakiwa wamepunga kutoka asilimia 32 hadi 20, zinatia moyo.

Tukiwa katika maadhimisho ya waathirika wa ajali yaliyofanyika jana, tunawiwa kusema ni hatua madhubuti iliyochukuliwa na vyombo vinavyojishughulisha na usalama barabarani pamoja na mwitikio wa Watanzania wote waliowezesha hali kuwa hivyo.

Tunaamini, kwa kasi ile ile, bado tunaweza kupunguza ajali hizi kwa kiasi kikubwa ilimradi kuwepo utashi wa kila mhusika.

Tumeshuhudia ajali hizi zikiacha kadhia kubwa kwa waathirika wakiwemo waliopoteza viungo, maisha na hata kuathiri ustawi wa familia kwa kiasi kikubwa.

Zipo familia zilizopoteza wazazi wote, watoto, ndugu, jamaa na marafiki na zimeathirika kwa kiasi kikubwa ikiwa ni pamoja kupoteza mwelekeo mahali ambapo ajali imemwondoa mtu ambaye ndiye alikuwa ni tegemeo na muhimili mkubwa wa familia husika.

Moja ya hatua iliyochukuliwa na vyombo husika hasa vya usalama barabarani ni kutoa elimu kwa wahusika.

Hapa tunalipongeza Jeshi la Polisi na taasisi nyingine zilizojitolea kutoa elimu kwa umma kikiwemo Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake (Tamwa).

Tamwa wamekuwa wakitoa elimu kwa waandishi wa habari ambao kwa kutumia vyombo vyao, wamefanyakazi kubwa.

Tamwa katika kutoa mchango wao wa kudhibiti ajali za barabarani imetoa mafunzo kwa wanahabari 142 ambapo kati yao, wanaume 69 na wanawake 73, pia wahariri 47 kati yao wanaume 28 na wanawake 19 huku wanahabari wa mtandao wa kijamii wakiwa 38 ambapo kati yao wanaume 24 na wanawake 14.

Pia kutoa elimu kwa vikundi na vyama vinavyojishughulisha na usafirishaji wa abiria na mizigo pamoja na kwa abiria wenyewe.

Tumeshuhudia Polisi wa Usalama Barabarani wakiwa wamechukua hatua ya kudhibiti madereva hasa waendao mikoani na wasafirishaji wa abiria na mizigo kwenda nchi jirani ambao kwa kawaida wanaendesha kwa mwendo wa kasi ili kuwahi waendako na badala yake wamekuwa wakiishia kuleta ajali barabarani.

Jeshi la Polisi kitengo cha usalama barabarani kwa kweli wamefanya mageuzi makubwa ikiwa ni pamoja na kuwashirikisha abiria kutoa taarifa popote walipo kwa makamanda wa mikoa na wilaya kwa kubandika namba zao kwenye magari makubwa ya abiria.

Tunaamini kwa pamoja, abiria, wasafirishaji wa abiria na mizigo, wamiliki wa vyombo moto vya usafiri pamoja na visivyokuwa vya moto wakiwemo watembea kwa miguu, tuheshimu sheria za usalama barabarani huku tukijikinga na ajali na kuwakinga wengine.

Columnist: habarileo.co.tz