Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

Tumsaidie Rais Samia kufikia malengo

Afc8763142b0820441c7b9d43770dc71.jpeg Tumsaidie Rais Samia kufikia malengo

Sat, 20 Mar 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

ALIYEKUWA Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan jana ameapishwa kuwa Rais wa Sita wa Tanzania baada ya kifo cha Dk John Magufuli kilichotokea Jumatano wiki hii mkoani katika Hospitali ya Mzena mkoani Dar es Salaam.

Rais Samia baada ya kula kiapo mbele ya Jaji Mkuu wa Tanzania, Profesa Ibrahim Juma, amewatoa wasiwasi

Watanzania kuwa hakuna kitakachoharibika baada ya kifo cha Dk Magufuli na kuwahakikishia kuwa taifa liko imara.

“Niwahakikishie kuwa tupo imara kama taifa, na sisi viongozi wenu tumejipanga vizuri kuhakikisha tunaendelea pale mwenzetu alipoishia,” alieleza Rais Samia, huku akiongeza kuwa huu ni wakati wa kudumisha amani, kuenzi utu, uzalendo na utanzania na si wakati wa kutazama mbele kwa mashaka, bali kutazama mbele kwa matumaini na kujiamini.

Tungependa kusisitiza kauli hii ya Rais Samia hasa wakati huu ambao Tanzania liko katika majonzi na maombolezo makubwa ya kuondokewa na mpendwa wetu, shujaa wetu Dk Magufuli. Sote tunakubaliana kuwa ni kipindi kigumu na jambo lililotokea Watanzania hawakulitarajia na kamwe hawakupenda litokee.

Lakini kwa kuwa Mwenyezi Mungu ndiye hupanga uhai wa mwanadamu, tunaungana na Rais Samia kusisitiza Watanzania kudumisha amani, uzalendo na utanzania wetu kwa kuendelea kuchapa kazi kwa bidii kwa nia ya kuhakikisha Tanzania inabaki salama na inasonga mbele kwa kasi.

Na hii itakuwa ni faraja kubwa kwa Dk Magufuli aliyetutoka kuona kuwa Tanzania aliyoiacha, inaendelea kuwa nchi ya amani, umoja na mshikamano, lakini kubwa zaidi kama alivyoeleza Rais Samia tunaijenga Tanzania mpya ambayo Rais Magufuli aliitamani siku zote kama alivyokuwa akieleza kwa miaka sita aliyokuwa madarakani.

Hili linawezeka endapo kila Mtanzania atajikita kuendelea kufanya kazi kwa bidii kwa nia ya kujenga uchumi wa mtu binafsi na wa taifa kwa ujumla, hasa tukizingatia maono ya Dk Magufuli, lakini zaidi na maelekezo ya Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ya 2020-25 ambayo ndiyo dira ya kufikia maendeleo tunayoyataka.

Ilani hii ambayo viongozi wa serikali wanaitekeleza hivi sasa imeweka mwongozo wa yote yanayopaswa kufanyika kwa kipindi cha takribani miaka minne na ushee iliyobaki ya awamu hii ya tano, hivyo ni vyema viongozi wakaendelea kusimamia kwa makini ili Tanzania ifanikishe malengo yaliyoainishwa humo.

Sisi hatuna shaka na tunaamini chini ya uongozi wa Rais Samia haya yanaweza kufikiwa kutokana na ukweli kuwa wakati akiwa Makamu wa Rais, alimsaidia Dk Magufuli kuifikisha Tanzania hapa ilipo ambako imekuwa nchi ya kupigiwa mfano siyo tu Afrika, bali duniani kote kutokana na kasi yake ya maendeleo.

Kwa hiyo, anapoanza urais wake huo rai yetu ni kwa kila Mtanzania kuanzia viongozi hadi wananchi wa kawaida, kumpa ushirikiano unaohitajika na kumuunga mkono katika uongozi wake ili Tanzania izidi kung’ara kimaendeleo.

Columnist: www.habarileo.co.tz