Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

Tuitumie kwa tija siku ya Uchaguzi Mkuu 2020

79579ad7a5b420bc20a68923880e11e7 Tuitumie kwa tija siku ya Uchaguzi Mkuu 2020

Sun, 18 Oct 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

WATANZANIA wapo katika siku za mwishomwisho za kampeni za Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2020 unaotarajiwa kufanyika Oktoba 28, 2020 kuchagua rais, wabunge na madiwani.

Kwa vyama vya upinzani, uchaguzi wa mwaka huu nao unatafuta fursa ya wagombea kutumwa Ikulu kuwatumikia Watanzania kwa mara ya kwanza.

Hali ni tofauti kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambacho mgombea wa urais, Rais John Magufuli anatetea nafasi yake kwa kipindi cha pili cha miaka mitano ijayo.

Hata hivyo, kutokana na ubora wa wagombea kwa namna walivyotumikia nafasi zao kwa nafasi mbalimbali, baadhi ya wananchi na wapiga kura, wameanza kusherehekea ushindi kwa wagombea wanaowaona bora kuongoza ama kwa udiwani, ubunge au urais.

Tunasema, baadhi wamesikika hata wakisema hawaoni sababu ya kujitokeza siku itakapowadia ili wapige kura kwa kuwa wanaamini mgombea wao ni bora kuliko wengine hivyo, iwe isiwe lazima atashinda.

Sisi tunasema, kufikiri na kutekeleza wazo la kutojikeza kupiga kura siku ikiwadia, ni potofu kwa kuwa linalenga kumnyang’anya kura mgombea mzuri unayemtaka, na kuipeleka kwa mgombea mbovu na asiye na sifa wala vigezo vya uongozi.

Ndiyo maana tunasema siku ya kupiga kura itapaowadia, yapo mambo muhimu kwa Watanzania wenye sifa za kupiga kura yawapasayo kufanya. Kwanza, ni kujua kwa dhati kuwa, kutokupiga kura ni kumpa ushindi mgombea usiyemtaka na kumyang’anya unayempenda kuwa kiongozi.

Aidha tunasema wakati wa kupiga kura, wapigakura waepuke kura za usaliti na za mihemuko na badala yake, wapige kura za kizalendo. Kwetu sisi, kura za usaliti ni zile za kumnyima anayefaa hata kama aliwahi kufanya na kuonekana anafaa, kwa sababu tu eti ni wa kabila, dini, mkoa, kanda au chama fulani cha siasa. Huu, ni usaliti kwa taifa.

Tunasema, kura za mihemuko, ni zile unazoweza kuwa na mapenzi makubwa kwa mgombea kiasi kwamba ukaenda kupiga kura, lakini ukalewa mapenzi na kujikuta umeharibu kura.

Kuharibu kura yako, ni sawa na kutokujitokeza kupiga kura kwa sababu kura uliyopiga na kuiharibu, haiwezi kuhesabika ili kumpa ushindi mgombea wako.

Yanayoweza kufanyika na kuharibu kura, ni pamoja na kuweka alama ya vema kwa mgombea unayemtaka, kisha ukaandika, ukachora au kuweka alama nyingine yoyote kwenye karatasi ya kura.

Kufanya hivyo, ni kuharibu kura; ni sawa na kutokupiga kura; ni kumpa ushindi mgombea usiyemtaka na kumnyima au kumnyang’anya mgombea unayependa ashinde na kuongoza.

Mambo au alama za ziada zisizotakiwa katika karatasi hiyo ni pamoja na kuweka alama yoyote, kuandika mambo au majina yako au ya mgombea yeyote wala chama chochote, na kuchafua au kuvuruga kwa namna yoyote picha, jina au alama yoyote katika karatasi ya kura.

Ni kosa. Ndiyo maana tunasema, bila umakini tutawapa ushindi wagombea tusiowataka na kuwanyang’anya tunaowapenda ndiyo maana tunasema, Oktoba 20, 2020 siyo siku ya kazi, siyo siku ya ibada, ni siku ya mapumziko, hivyo tuitumie kwa tija kujityokeza kupiga kura kwa makini kupata viongozi tuwatakao.

Columnist: habarileo.co.tz