Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

Tuchangie kuimarisha uchumi wetu

6a6a0bf74daf33fb79cd961388f5c775 Tuchangie kuimarisha uchumi wetu

Fri, 11 Jun 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

WAZIRI wa Fedha na Mipango, Dk Mwigulu Nchemba jana aliwasilisha bungeni taarifa ya Hali ya Uchumi wa Taifa kwa mwaka 2020, na kueleza kuwa licha ya mlipuko wa Covid-19 ulioathiri uchumi wa nchi, Tanzania ni miongoni mwa nchi chache duniani zilizokuwa na ukuaji chanya wa uchumi huku Pato la Taifa likikua kwa kwa asilimia 4.8.

Alizitaja sekta zilizokua kwa viwango vya juu kwa mwaka 2020 ni Ujenzi (asilimia 9.1), Habari na Mawasiliano (asilimia 8.4), Uchukuzi na Uhifadhi wa Mizigo (asilimia 8.4), Huduma zinazohusiana na Utawala (asilimia 7.8), shughuli za kitaalamu, sayansi na ufundi (asilimia 7.3), Madini na Mawe (asilimia 6.7) na Afya na Huduma za Jamii (6.5%).

Dk Mwigulu amesema taarifa ya Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) ya Aprili 2021 inaonesha kuwa mwaka 2020 dunia ilikuwa na mdororo wa uchumi kwa kupata ukuaji hasi wa asilimia 3.3 ikilinganishwa na ukuaji chanya wa asilimia 2.8 mwaka 2019. Amesema ukuaji hasi ulisababishwa na kupungua kwa shughuli za kiuchumi duniani hususan, biashara, usafirishaji na utalii kutokana na mlipuko wa Covid-19.

Amefafanua kuwa mwaka wa fedha 2021/2022, serikali imeweka malengo na shabaha za kiuchumi sita ikiwamo ya kuongeza kasi ya ukuaji wa Pato Halisi la Taifa kufikia asilimia 5.6 mwaka 2021.

Ukiangalia takwimu hizi zilizotolewa na Waziri wa Fedha na Mipango unaona dhahiri jinsi serikali ilivyo makini kuona kwamba hali ya uchumi nchini inaimarika na inazidi kuimarika siku hadi siku, na uthibitisho ni ukuaji chanya wa uchumi licha ya kukabiliwa na ugonjwa wa virusi vya corona.

Tunaamini mipango iliyowekwa na serikali kupitia Taarifa ya Hali ya Uchumi ya mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa wa mwaka 2021/22, inaonesha dhahiri kuna matarajio makubwa ya kukua kwa uchumi na hasa kama kila mmoja atatoa mchango wake kuhakikisha hilo linafanikiwa.

Hakuna shaka kwamba kutokana na kazi nzuri ambayo ilifanyika kwa miaka mitano iliyopita kabla ya kuzuka kwa virusi vya corona, ukuaji wa uchumi wa Taifa ulikuwa wa hali ya juu na ilikuwa miongoni mwa nchi zenye uchumi unaokua kwa kasi kwa takriban asilimia 6.5 hadi asilimia saba.

Kwa msingi huo, ni vyema kila Mtanzania na kila mwenye kupenda maendeleo akajitolea kwa nguvu zake katika eneo lake la kujiletea kipato ili kuchangia katika kukuza uchumi ambao unapoimarika, huduma nyingi zinaimarika na hivyo Watanzania wengi kufaidika na matunda ya hali nzuri ya uchumi.

Na hili litawezekana kutokana na ukweli kuwa Watanzania kama alivyokuwa akipenda kusema Rais wa Serikali ya Awamu ya Tano, Dk John Magufuli, hawana mjomba, kazi ndiyo kila kitu, hivyo kila mmoja atimize wajibu wake kikamilifu ili nchi isonge mbele.

Columnist: www.habarileo.co.tz