KOCHA wa timu ya soka ya waandishi wa habari za michezo wanawake, Rahel Pallangyo, amesema maandalizi ya mchezo wa kirafiki dhidi ya wachezaji wanaocheza Ligi Kuu Tanzania Bara unaotarajiwa kuchezwa Uwanja wa Karume, Dar es Salaam, Agosti 23, yanaendelea vema.
Akizungumza jana katika mazoezi yaliyofanyika Uwanja wa Karume, Dar es Salaam, Rahel alisema mashabiki watarajie kuona burudani ya kusisimua katika mchezo huo.
“Wachezaji wamejitoa na wanawahi mazoezini saa 12:00 alfajiri, inaonesha wamedhamiria kuonesha vipaji vyao vingine licha ya kuandika na kutangaza michezo pia wanajua kuucheza mpira,” alisema kocha Rahel.
Pia kocha huyo alijivunia wachezaji wake kama Winniyah Maulid, Esta Maongezi, Mwanaid Suleiman, Devota Kihwelo, Salama Ngare, Victoria Mungure, Lucy Mgina, Rehema Lucas, Salma Seif na makipa ni Martha Mbona na Pendo Pamba.
Alisema wachezaji wa timu yake wameonesha kiwango cha kikubwa kiasi cha kocha wa timu ya Taifa ya wanawake, Edna Lema, kuvutiwa na baadhi yao.
‘Kocha Edna amekuja kusaidiana na mimi na kukubali baadhi yao na kusema wanaweza kucheza ligi ya ushindani japo wanahitaji marekebisho madogo madogo,” alisema
Naye timu meneja wa timu hiyo, Victoria Mungure, alilishukuru Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kwa kuwapatia uwanja na vifaa vya mazoezi.
Aidha, Victoria alisema wanatarajia siku ya mchezo kutakuwa na ugeni mkubwa ambao wameunga mkono jitihada za waandishi hao kuibua hamasa ya soka la wanawake nchini.