Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

Serikali kununua ndege nyingine 5

C39ea4d31e6266d5bc50e0b78524b871 Serikali kununua ndege nyingine 5

Mon, 2 Aug 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

SERIKALI imesaini mkataba wa kununua ndege mpya tano, zikiwamo mbili za masafa marefu.

Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa alisema jana Dar es Salaam kuwa, kati ya ndege hizo za masafa marefu, moja ni ya mizigo na nyingine ya abiria.

Msigwa aliwaeleza waandishi wa habari kuwa, juzi serikali ilipokea ndege ya tisa kati ya 11 mpya na nyingine mbili zitaingia nchini kabla ya mwisho wa mwaka huu.

Alisema hayo wakati akitoa taarifa ya kipindi cha robo ya mwaka ya mwaka wa fedha kilichoanza Aprili na kuishia Juni, mwaka huu.

Msigwa alisema ndege ya masafa marefu itakuwa na uwezo wa kubeba abiria 260.

“Tunanunua ndege nyingine mpya tano, ATCL wameshasaini mkataba na kampuni moja ya kutengeneza ndege, lengo letu tununue ndege kubwa ya masafa marefu moja na nyingine kubwa ya mizigo, tumepata soko hata la mazao na mbogamboga hivyo lazima tuwe na uhakika wa usafiri ili visiharibike,” alisema.

Alisema ndege nyingine mbili zitakuwa za masafa ya kati zenye uwezo wa kubeba abiria kati ya 160 hadi 170 na ndege nyingine itakuwa ya kubeba abiria 76.

Alisema faida za ndege hazipimwi kwa kuangalia makusanyo ya tiketi zilizouzwa, ila ufanisi wa huduma na uwezo wa kuhudumia maeneo mengi.

“Tunataka Tanzania ikue na kuwa kivutio cha utalii wa afya, tunaendelea kuboresha sekta ya afya na sasa tunaboresha zaidi sekta ya usafiri, kwa sababu ukiwa na ndege za kutosha na mtu akitaka kuitembelea Tanzania, anaangalia usafiri wa anga ukoje, je anaweza kusafiri eneo moja kwenye jingine kwa usafiri huo?, je huduma hiyo ipo, ndio anapanga safari yake kuitembelea, akiona hakuna usafiri wa uhakika hawezi kuja,” alisema Msigwa.

Hivi sasa Tanzania ina ndege kubwa moja ya masafa marefu Boeing 787-8 Dreamliner yenye uwezo wa kubeba abiria 262, ndege nyingine Airbus 220-300 tatu za masafa ya kati, na nne aina ya Bombadier Q 400 za masafa mafupi zenye uwezo wa kubeba abiria 76 kila moja.

Julai 30, mwaka huu Rais Samia Suluhu Hassan alipokea ndege ya tisa aina ya DE Havilland DASH 8-Q400 itakayotumika kwa masafa mafupi.

Columnist: www.habarileo.co.tz