Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

SIO ZENGWE: Si vyema Karia, wachambuzi kucharurana

Rais Karia Rais wa TFF, Wallace Karia

Tue, 8 Mar 2022 Chanzo: Mwanaspoti

Wiki iliyopita iliisha vibaya baada ya Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Wallace Karia kurusha kombora kwa wachambuzi wa soka ambao hivi sasa wamekuwa wengi, wakisifiwa na kupondwa.

Katika moja ya hafla, Karia alisema wachambuzi wanatakiwa kwenda kusoma kwanza kabla ya kurudi kufanya kazi hiyo ya uchambuzi “wa kila kitu” kuanzia mechi hadi masuala mengine ya maendeleo ya michezo.

Kauli hiyo imesababisha wachambuzi wahamaki na kutoa maneno makali kumjibu Karia, ambaye pia alizungumzia masuala mengine mengi, ikiwemo michuano ya mitaani, maarufu kwa jina la Ndondo ambayo kiutamaduni ilikuwa ikifanyika wakati msimu umeisha ili kuwapa nafasi wachezaji nyota wa klabu kubwa kurudi nyumbani kuungana na vijana wa mitaani kwao katika timu ambazo hazijasajiliwa.

Nimefuatilia mjadala na malumbano hayo, nikaona yanaelekea sehemu ambayo haiwezi kusaidia mpira wetu zaidi ya kupata mshindi katika malumbano. Na ushindi wake si muhimu kwa maendeleo ya mpira na badala yanaweza kutujengea imani potofu itakayochangia zaidi kuuporomosha.

Namuelewa Karia kwa kuwa alikuwa kiongozi wangu. Naelewa jinsi anavyozungumza na jinsi ambavyo anaweza kutoka nje ya mstari wakati anataka kueleza jambo muhimu sana.

Nakumbuka kule Arusha kwenye Mkutano Mkuu aliwahi kutamka neno ambalo lilitafsiriwa kuingiza siasa katika soka alipokuwa akiponda wapinzani. Nia yake ilikuwa kutaka kuzungumzia madhara ya upinzani usio na maana au usio muhimu, lakini akajikuta anataja majina ya wanasiasa.

Na nahisi katika hili la wachambuzi alitaka kumaanisha kusomea mifumo, falsafa na mambo muhimu katika mchezo, uongozi, biashara na mambo mengine ya soka.

Pengine anadhani wachambuzi wanahitaji ufahamu zaidi wa masuala yanayozunguka soka ili waweze kufanya kazi yao bila ya kuegemea upande mmoja au kuweka mbele maslahi binafsi.

Wenzetu hutumia watu waliowahi kucheza mpira kuchambua mechi kwa sababu hawa wanakuwa wamepitia chini ya walimu tofauti wenye ujuzi tofauti na pia mambo yanayozunguka maandalizi ya mchezo na hali ya mchezo yenyewe.

Hivyo, hawa si kwamba wamesomea kuwa wachambuzi bali wana ufahamu wa kutosha kuhusu mchezo na mechi zenyewe.

Hali kadhalika kwa viongozi au au waliojikita katika masuala ya uongozi huitwa kutoa maoni yao kuhusu masuala ya uongozi pale matatizo yanapotokea au mazuri yanapotokea. Vivyo hivyo kwa waamuzi na watu wa fani nyingine. Baadhi huwa wamesomea eneo wanalotoa maoni na wengine huwa na uzoefu na masuala yanayohusu eneo hilo.

Na wote hawa hawaajajiriwa kwa kutoa maoni au kuchambua, bali pengine hulipwa posho ya kulipia muda waliotumia kukaa studio au mafuta waliyotumia kwenda eneo la kuhojiwa.

Nitamani iwe na pengine ndicho alichomaanisha Karia ambacho kimetafsiriwa kama dongo kwa wachambuzi.

Kama nilivyowahi kuandika huko nyuma, uchambuzi ni muhimu katika uendeshaji mpira kama zilivyo sehemu nyingine kwa kuwa unasaidia viongozi, wachezaji, mashabiki na wadau wengine kuwa na ufahamu mpana wa kile wanachokifanya au kukipenda.

Na sio hilo tu, muda wanaotumia kujadili soka, unatangaza zaidi mchezo huo na hivyo umuhimu wao hauwezi kupuuzwa au kudhihakiwa.

Ndio! Kumekuwa na lawama nyingi kwa wachambuzi pengine kutokana na masihara wanayofanya wanapochambua, misimamo wanayoiweka badala ya kuhifadhi maneno. Mfano mtu anasema anaamini; “Hakuna mchezaji wa timu fulani mwenye uwezo wa kuchezea timu nyingine.” Hii ni dhahiri kuwa utaudhi mashabiki wa timu hiyo.

Mingine ni mijadala isiyo na kichwa wala miguu ya kulingankisha makocha au wachezaji, baadhi wakiapa kuwa fulani ndio bora hata kwa nini.

Hivyo, kama Karia anaungana na fikra hizo, alifikirie TFF ifanye nini kuboresha uchambuzi wao na kupata mafunzo mafupi ili kuwawezesha kupata ufahamu mkubwa wa uendeshaji mpira ili wachambue kwa usahihi zaidi na kuusaidia mchezo badala ya kutafuta majukwaa ya kucharurana.

Columnist: Mwanaspoti