Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

Pole sana Rais Magufuli

Ee22510e145503c2c7c18ca0d0ac07a6 Pole sana Rais Magufuli

Wed, 29 Jul 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

RAIS John Magufuli jana aliwaongoza Watanzania kutoa heshima za mwisho kwa mwili wa Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin William Mkapa aliyefariki dunia Julai 23, mwaka huu.

Mwili wa Mzee Mkapa ulianza kuagwa Julai 26, mwaka huu kwenye Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam na kuhitimishwa jana ambako pamoja na Rais Magufuli na familia ya Mzee Mkapa, viongozi wengine wakiwemo Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk Ali Mohamed Shein, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Burundi, Alain Guillaume Bunyoni na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Idd walipata fursa ya kutoa heshima za mwisho.

Mbali ya hao, viongozi wengine wakiwamo maspika, majaji wakuu, marais wastaafu, mawaziri wakuu wastaafu, mabalozi na wawakilishi wa mashirika ya kimataifa, viongozi wa dini, wa vyama vya siasa na wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama, walipata nafasi ya kumuaga Mzee Mkapa aliyeiongoza Tanzania kwa miaka 10 kuanzia 1995. Katika salamu zake, Rais Magufuli amesema Taifa limepoteza mtu aliyetoa mchango mkubwa katika kuleta mageuzi makubwa ya kiuchumi, kuimarisha huduma za kijamii (elimu, maji, afya), kuanzisha na kuimarisha taasisi muhimu za serikali, kuimarisha sekta binafsi na kujenga miundombinu hasa barabara na madaraja.

Pia kuinua ukusanyaji wa kodi, kuimarisha uhusiano na ushirikiano wa kimataifa, ukombozi na utatuzi wa migogoro ya mataifa mbali mbali ya Afrika na aliyekuwa mahiri katika kuibua vipaji vya viongozi akiwemo yeye mwenyewe, Rais Mstaafu Kikwete, Rais wa Zanzibar, Dk Shein na Mgombea wa Kiti cha Urais wa Zanzibar, Dk Hussein Ali Mwinyi.

Rais Magufuli amebainisha kuwa Mzee Mkapa ameacha mengi mazuri ya kujivunia na kuendelea kujifunza yakiwemo uongozi bora uliosimamia umoja, mshikamano, uchapakazi, uzalendo, uwajibikaji, uwazi na uhusiano mzuri wa kimataifa na ameahidi kuwa serikali anayoiongoza itafanya kila liwezekanalo ili kudumisha na kuendeleza mambo yote mazuri yaliyoasisiwa naye.

Tunampa pole nyingi Rais Magufuli kutokana na ukweli kwamba Watanzania kama alivyoeleza tumempoteza kiongozi mahiri, ambaye ametoa mchango mkubwa katika mageuzi makubwa ya sekta mbali mbali kama alivyozieleza kwa kina jana wakati wa hotuba yake.

Ni mageuzi hayo ambayo leo hii yamewafanya Watanzania watembee kifua mbele kwa sababu yameleta mabadiliko makubwa katika maisha ya watu, kiasi kwamba hayawezi kufutika katika kumbukumbu zao.

Na hilo linathibitishwa na jinsi watu walivyojitokeza kwa wingi kumuaga Mzee Mkapa pamoja na kumlilia lakini wakitoa sifa zake nyingi, ambazo hakika zinastahili kwa kiongozi wetu huyu tunayemzika leo.

Columnist: habarileo.co.tz