SUALA la viongozi wengi wa kisiasa na sekta nzima ya siasa kuonekana kama matunda ya rushwa kunakilazimisha Chama Cha Mapinduzi na serikali ya awamu ya tano, kupambana na kuong’oa shina la saratani ya ufisadi kwenye uchaguzi ambako ndiko kulikokuwa na mizizi ya janga hilo.
Ni ukweli kuwa madiwani, wabunge wa majimbo, viti maalumu na hata wajumbe wengine wa ngazi mbalimbali za kisiasa kwenye vyama walikuwa wanahusishwa na madai kuwa ni matunda ya rushwa ni kwa sababu wanapatikana kwa kutoa fedha na mali ili kununua wajumbe wanaohusika na kuchuja, uteuzi wa wagombea lakini pia na wapigakura ili wawachague.
Rushwa ya ngono nayo kwa kinamama ilichafua uwanja wa siasa. Wanadaiwa walikuwa wanatoa miili kwa wanaohusika na kupendekeza na kuteua wagombea wa viti maalumu na hata kwenye majimbo.
Jambo hili lilisababisha uongozi wa vyama, mihimili mingine ya dola kuchafuka kwa ufisadi kwa kuwa kilichozaliwa kwa njia haramu nacho bila shaka ni haramu na ndivyo hali ilivyokuwa.
Rushwa iliota mizizi ikianzia vijijini kwa kuchafua na kuharibu maadili ya viongozi, kuliingiza taifa kwenye tamaa za viongozi na wananchi kuchukua chao mapema.