Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

Nawasalimu kwa jina la Jamhuri  ya Muungano wa Tanzania

2b45dbc3da3df9ba31f57eb90187e2f1 Nawasalimu kwa jina la Jamhuri  ya Muungano wa Tanzania

Wed, 7 Apr 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

WAPENZI wasomaji wa gazeti hili na Watanzania wote, leo nimependa nianze kwa salamu mpya ambayo ametuanzishia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan.

Kwangu mimi meona salamu hii ni ya kizalendo na ya kimkakati ambayo ina mashiko mapana iwapo watanzania wataitumia kwa kumaanisha maana yake halisia.

Kimsingi salamu hii inalenga kudumisha Muungano wetu, kuboresha umoja wetu sote kama watanzania na kutufanya tushikamane katika kamba moja kama Watanzania. Lakini kiitikio chake kwamba ‘kazi inaendelea’ pia kinapeleka ujumbe muhimu kwa wananchi kwamba lazima tuendelee kuchapa kazi na kama sehemu ya kumuenzi Hayati John Magufuli na falsafa yake ya ‘Hapa Kazi Tu’.

Dhana ya Muungano wa Tanzania ni pana sana na wakati mwingine baadhi ya wanasiasa wamekuwa wanaitohoa tofauti na kutengeneza mkanganyiko kwa wananchi.

Je, salaamu hii inalenga kuwafumbua macho wanasiasa uchwara hao? Je, tutaitumia vyema kama watanzania na kudumisha na kuenzi muungano wetu kwa upendo na umoja mkuu?

Natambua maandiko matakatifu yanasema ‘amri kuu nawapa mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo.’ Yohana 13:34.

Maneno haya aliyasema Yesu kwa wanafunzi wake. Kwa mtazamo mwepesi maneno haya yanaendana na salamu ya Mheshimiwa Rais aliyoianzisha, ambayo kimsingi ilikuwepo tu bali hatukuwahi kuwaza kuitumia tunapokutana na hususani katika mihadhara.

Nakumbuka maneno yake katika hotuba aliyoitoa pale Dodoma wakati wa msiba wa kitaifa wa Hayati Dk Johh Magufuli alipowataka watanzania waondoe hofu kwa kuwa hakuna kitakachobadilika wala kuharibika.

Inawezekana akina Thomaso tulikuwa wengi kutokana na hofu illiyokuwa imetanda wakati ule ya kuondokewa na jabali, chuma au tingatinga, aliyekuwa Rais wetu, Dk Magufuli.

Lakini baada ya kumteua na kuthibitishwa na Bunge Makam wa Rais, Dk Philip Mpango illiwafanya watanzania wajawe na furaha kufuatia uteuzi huo maridhawa.

Furaha hii ilitokana na imani watanzania walio nayo dhidi ya Rais wetu, Mama Samia na Dk Mpango ambaye ni mbobezi katika masuala ya uchumi. Imani hii ilijengeka tangu miaka zaidi ya mitano iliyopita wakati wa Dk Maguulli hadi Mama Samia kushika hatamu.

Pamoja na mambo mengine, dhana ya kushikamana na kuzidisha umoja na mshikamano ndiyo umekuwa wimbo mkuu wa viongozi hawa wa nchi yetu. Kwa nyakati tofauti Rais Samia ameonyesha pasi na shaka ahadi yake ya kuendeleza kile alichokianzisha Hayati Dk Magufuli.

Natambua kuna baadhi ya wanasiasa uchwara watakaombeza na kunyambua teuzi za Rais Samia lakini ukweli utabaki kuwa hata siku moja hakuna kitakachofanyika na kukubalika kwa wote.

Jambo la msingi ni kuzidi kushikamana kama watanzania na kumuunga mkono Rais wetu katika kuwaletea maendeleo watanzania wote.

Nilifurahishwa na hotuba yake wakati wa kuapisha mawaziri na katibu mkuu kiongozi alipowataka viongozi hao wote kufanya kazi kwa umoja, kushirikiana bila kudharauliana.

Dhana hii ni pana sana. Kuna nyakati baadhi ya mawaziri wamekuwa wakiendesha shughuli zao kwa utengano kana kwamba wote hawajengi mama Tanzania mmoja.

Nafikiri hichi ndicho alichomaanisha Mama yetu Samia alipowataka washirikiane kwa kila namna kuitetea serikali na kuwatumikia watanzania wote.

Utawala huu unaonyesha kuwa utawala utakaotumia maarifa sana kuliko kutumia nguvu. Na kwa vile Magufuli alikuwa mwanadamu na kwa kuwa kila mwanadamu ana mapungufu yake basi kama yalikuwepo machache utawala wa Mama Samia utayarekebisha.

Kwa maelekezo ya Rais ni wazi kwamba wafanya biashara watakuwa huru kuendesha kazi zao bila funga funga kwa sababu ya kodi.

Rais Samia ni wazi kwamba anatamani kuona kila mtanzania akiipenda nchi yake kwa moyo wake wote na hii ni pamoja na kulipa kodi kwa hiari na kwa mujibu wa taratibu zilizopo pasipo kubambikwa wala kukomolewa.

Je, wafanyabiashara wetu wataelewa lengo la kiongozi wetu huyu wa mama Tanzania? Dhana ya rushwa mara nyingi imeonekana kupingwa na kila kiongozi wa nchi hii. Kwa kauli ya Rais Samia na Makam wake Dk Mpango inaonyesha dhahiri kabisa kwamba wamepanga kupambana na kirusi hiki bila kulegeza alipoishia Dk Magufuli bali kusonga mbele.

Ili nchi yetu iendelee suala la ukusanyaji kodi haliepukiki. Tena utoaji kodi pasipo shuruti ni jambo bora na jema zaidi.

Je, watanzania tunaelewa jambo hili? Je, tuko tayari kufanya hivyo? Haya ni maswali ya msingi tunayopaswa kujiuliza kama watanzania hasa kwenye kipindi hiki kinachohitaji umoja na mshikamano.

Mshikamano huu katika kulipa kodi huku tukiunga mkono serikali na ndiyo utakaosaidia huduma za maji kwa wananchi, utasaidia huduma za afya kwa jamii yetu na itasaidia kumaliza miradi ya maendeleo yote.

Kwa namna fulani hii inaendana na maneno ya Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere kwenye hotuba yake ya mwaka 1963 aliposema:

“Ninapoulizwa kwa mfano, ni nini mwezi wa Machi kwa muda wa siku mbili tu, jibu langu ni moja, umoja. Wenzangu na mimi tulikuwa kitu kimoja. Na tulikuwa kitu kimoja kwa sababu Tanganyika (kwa sasa Tanzania) yenyewe ni kitu kimoja. Na vile vile katika mambo yetu yote ya maisha ya taifa letu. Nani asiyejua kwamba msingi wa kufanikiwa kwa TANU, ni umoja wa TANU?

“Kadhalika katika vyama vya ushirika au vyama vya wafanyakazi wanachama wake wanaposhikana bega kwa bega, mambo yao yatawaendea vyema. Wanachama wake wakigombana na kutengana, mambo yao na mambo ya taifa zina yatakwenda tenge. Ndugu zangu, huu si wakati wa kuchezea umoja wetu, tunauhitaji sasa kama tulivyouhitaji zamani kwa ajili ya kuinua hali zetu na ndugu zetu.”

Nadhani huu ni wakati mwafaka kwa watanzania kutumia salamu hii mpya ya Rais wetu kwa maslahi mapana ya watanzania siyo tu kama mazoea bali kumaanisha ujumbe mzito uliyo ndani mwake na Mungu atusaidie.

: +255 712 246 001; HYPERLINK "mailto:[email protected]" [email protected]

Columnist: www.habarileo.co.tz