Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

Mawaziri wenye tamaa ya urais ni kikwazo kwa Rais

Uwaziripic Mawaziri wenye tamaa ya urais ni kikwazo kwa Rais

Thu, 30 Sep 2021 Chanzo: mwananchidigital

Tuanze hapa; kuna tofauti kubwa kati ya ndoto na tamaa. Mwenye kuota huwa na subira, huamini wakati wake sahihi utafika. Aliyejawa tamaa, huona zamu yake inachelewa.

Kuelekea Uchaguzi Mkuu Kenya Agosti 2022, yapo majina mawili yanatawala; Raila Odinga na William Ruto. Kuna mmoja ana ndoto, mwingine ni mwenye tamaa kubwa. Nitafafanua!

Raila ana ndoto, ndio maana mwaka hadi mwaka anagombea urais, anashindwa, lakini anabaki na subira. Ruto ana tamaa. Ikawa sababu ya kutoelewana na Rais Uhuru Kenyatta, kisa ukaribu wake na Raila.

Uhuru na Raila walipofanya maridhiano na kufanikisha Mpango wa Ujenzi wa Daraja (BBI), kwa ajili ya kuzika uhasama wa kisiasa, Ruto akakasirika. Akaona Uhuru anataka kumbeba Raila kwenye uchaguzi ujao Kenya.

Wakati Uhuru alikuwa akijitetea kuwa ukaribu wake na Raila sio wa kisiasa, bali ni kwa masilahi ya Kenya na Wakenya. Ruto hakuelewa maelezo hayo. Ni kwa sababu fikra zake zilikuwa zinawaza urais kuliko chochote.

Hapo ndipo kwenye elimu ya msingi; kwamba mtu mwenye tamaa ya urais, hata akiwa sehemu ya Serikali yenye Rais mwingine, hufanya mambo kwa ajili ya kujisafishia njia kwenda Ikulu kuliko kuitumikia nchi inavyopasa.Huu ndio ujumbe ambao nimekusudia kumfikishia Rais Samia Suluhu Hassan. Ndani ya Serikali anayoiongoza, Baraza la Mawaziri, anaweza kuwa na maadui, ingawa hawatajipambanua mbele yake. Inawezekana akawaamini lakini watamwangusha.

Rais Samia anatakiwa kuwabaini mawaziri wenye tamaa ya urais na kuwaweka kando, kisha ajitenge nao kabisa. Hawatamsaidia yeye kama rais na taifa, bali siku zote itakuwa kujionesha ili kujisafishia njia ya kushika mpini.

Akumbuke jinsi watu walivyoshughulikiana nyakati za mwisho wa urais wa Alhaj Ali Hassan Mwinyi, vita ikawa kubwa kuelekea kumrithi Rais wa Tatu, Benjamin Mkapa, vivyo hivyo wakati wa kumpokea kijiti Rais wa Nne, Jakaya Kikwete.

Hili sio la Tanzania tu, mfano upo kwa Uhuru na Ruto, hawaelewani. Rais wa Pili wa kidemokrasia Afrika Kusini, Thabo Mbeki, alivurugana na Makamu wake, Jacob Zuma. Mbeki Rais, halafu kuna msaidizi wake anautaka urais, pakachimbika. Mbeki akalazimishwa kujiuzulu. Zuma akaingia.

Rais akiwa na msaidizi mwenye tamaa ya urais, hawezi kuwa na uaminifu wa kuitetea serikali. Machoni kwa rais anaweza kutoa kila aina ya sifa, pembeni atamponda kiongozi wake kwamba hawezi kazi.

Kipo kiburi hujengeka kwa mwenye kuusaka urais. Hujiona yeye ndiye anayeweza kazi kuliko hata aliyepo madarakani. Na kwa kawaida huwezi kumwongoza mtu anayejiona ana uwezo mkubwa kuliko wewe.

Suala la rais kufanya kazi na wapinzani wake ndani ya Serikali anayoiongoza, lipo pia kwenye kitabu cha “Team of Rivals: The Political Genius of Abraham Lincoln” – “Timu ya Wapinzani: Maarifa ya Kisiasa ya Abraham Lincoln.”

Mwanahistoria wa Marekani, Doris Kearns Goodwin, kupitia kitabu hicho, aliandika kuhusu serikali iliyoundwa na Rais wa 16 wa nchi hiyo, Abraham Lincoln, kwamba alifanya kazi na watu ambao walikuwa na ndoto ya kupata urais.

Washindani wa Lincoln wa kisiasa ambao walikuwepo kwenye Baraza la Mawaziri aliloliunda ni Waziri wa Fedha, Salmon Chase, Waziri wa Mambo ya Nje, William Seward, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Edward Bates. Hao ni kuwataja kwa uchache.

Shida kubwa kwa mawaziri wenye uchu ya urais ni kutengeneza makundi. Utakuta mpaka Serikali inapita vipindi vyenye joto kali, kisa makundi ya wasaka madaraka. Rais Samia akitaka uongozi wake usipitie joto hilo, ajitenge na asiwape nafasi wote wenye tamaa ya urais. Waliopo awatoe.

Urais hauji kwa nguvu

Uongozi huletwa na Mungu, japo jitihada hazikatazwi. Samia hakuwahi hata kujitokeza kugombea urais, lakini leo ndiye Amiri Jeshi Mkuu. Alipewa nafasi kwa kuwa mgombea mwenza, akawa Makamu wa Rais, kisha ikampendeza Mungu kumtwaa Rais John Magufuli.

Mwinyi (baba) na hata mwanawe, Hussein Mwinyi, hawakuwahi kujipambanua popote kutaka urais, lakini utulivu wao uliwezesha kupendekezwa. Hata Mkapa, hakupata kujionesha mwenye tamaa ya urais, lakini muda ulipofika aligombea na kupata. Kadhalika, Magufuli.

Kikwete, mwaka 1995, hakutaka kujitokeza kugombea urais. Alitaka kutulia na uwaziri.

Columnist: mwananchidigital