Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

Matano ya kumbukumbu za Mwalimu Kashasha

Kashashaaa Aliekuwa Mchambuzi wa Masuala ya Soka, Mwalimu Kashasha

Mon, 23 Aug 2021 Chanzo: www.mwanaspoti.co.tz

Kila nafsi itaonja mauti. Katikati ya wiki tasnia ya habari na michezo ilipata pigo kwa kuondokewa na mwalimu na mchambuzi mahiri wa michezo hususan soka, Theogenes Alex Kashasha maarufu Mwalimu Kashasha.

Kashasha alikuwa mmoja wa wachambuzi walioandikia Mwanaspoti akiwa na kolamu ya Kwako Mwalimu Kashasha iliyokuwa ikitoka kila Jumamosi ukurasa wa 12 na pia alichangia maoni tofauti gazetini.

Kupitia makala hii wakati tunaendelea kumuenzi Mwalimu Kashasha, Mwanaspoti linakuletea mabao matano ambayo Kashasha alitangaza kwa ufundi zaidi enzi za uhai wake akiwa TBC.

FEITOTO VS MWADUI

Bao la Feisal Salum ‘Feitoto’ Januari 15, 2019 kwe-nye U-wanja wa Benjamin Mkapa, Dar dhidi ya Mwadui FC ni miongoni mwa yale yaliyotangazwa na Kashasha. Feitoto alifunga bao la tatu kwa Yanga katika dakika ya 57 kwenye ushindi wa mabao 3-1.

Kashasha alilitangaza bao hilo kwa maneno haya:

“Unajua football ina maajabu yake. Football ina flavour. Haya ndiyo mambo yanayomfanya mtu anayependa mpira basi atamani kwenda kiwanjani. Ukiangalia Yanga kama walitaka kukosea ile move baada ya Ajib Ibrahim kupiga locomotive faint in combination na real faint, beki akaenda kuchukua ule mpira lakini akang’ang’ana sana kwa sababu ni mzuri kwenye nguvu za miguu, akaipiga break diagonal pass kama vile inatambaa -’low scatter down pass’ ikamkuta Feitoto akapiga semi bending spinning ball ni kama sentimita saba kutoka kwenye krosi mpaka mtambaa panya. Ni bonge la bao. Ni goli moja zuri mno. Sioni tofauti ya bao la Ajib la faulo na bao la Feitoto, tofauti ilikuwa ni moja ile ilikuwa ni set piece na huu ni mpira ambao ulikuwa unatembea ‘mobile ball au moving ball.”

KAGERE VS YANGA

Bao lingine lilonogeshwa vyema na Kashasha ni lile lililokuwa pekee la Simba na la ushindi kwenye mchezo dhidi ya Yanga, Februari 16, 2019 likifungwa na Meddie Kagere kwa kichwa dakika ya 71 akimalizia pasi ya John Bocco. Kashasha akitangaza redioni (TBC) akisema:

“Lakini safari hii unaweza kuona pasi ndefu kutoka mstari wa katikati unaoitwa option line, ilipigwa high ball na Jonas Mkude upande wa Mashariki ya uwanja akamtupia Bocco Emmanuel akauweka chini, akascrean ule mpira, akapiga turn - akageuka, akamuacha Dante kule harafu akakomba ule mpira kwa maana akauchop ukaja kama unadondoka kwenye penalt box. Alichokifanya Meddie Kagere alishafanya hesabu akajua vyovyote vile golikipa ataucheza mpira ule, akacheza side flick head - ule mpira ukaenda golini kwa spidi ndogo mno, lakini kwa viwango vya kutosha bila mpira kwenda juu ya mtambaa wa panya wala bila kwenda kwenye miguu ya mabeki wa Yanga, kwako Jesse John..”

LAMINE MORO VS MBEYA CITY

Hii ilikuwa mechi ya Septemba 13, 2020 kati ya Yanga na Mbeya City ambapo Mwalimu Kashasha alitangaza bao pekee la Yanga lililofungwa kwa kichwa na Lamine Moro na kuwapa Yanga ushindi. Kashasha alilitangaza hivi:

“Staili ya Carlinhos ya kupiga faulo, huyu atakuwa ni specialist wa dead balls, alinyanyua moja nzuri, kimo cha Lamine Moro na Michael Sarpong akawa anatokea Lamine Moro upande wa Magharibi, akapishana nao the opposite direction kama anakimbia D Movement au D runs aka-uspy kule side spiking usawa wa paji la uso kwenye jicho lake la kulia, ngoma ikaenda usawa wa kamba nusu mita kutoka kwenye mtambaa panya - bonge la bao, mpira uliopigwa ni mkali, kichwa kilichopigwa ni kizito, golikipa angejitingisha nafikiri angekuta umeshatua chini kwenye kamba, kwako Jesse John..””

MORRISON VS SIMBA

Pia, bao la faulo la Benard Morrison akiwa Yanga aliloifunga Simba kwenye mechi ya Machi 8,2020 katika Uwanja wa Benjamin Mkapa linaingia kwenye matano bora aliyotangazwa Kashasha. Kupitia redio ya Taifa, TBC alitangaza hivi:

“Wanasema kwenye kichwa cha kawaida binadamu yeyote ana skills zake, lakini hii ni top of mental skills ukiongeza na ubunifu kwa sababu alichokifanya ni utulivu mkubwa sana. Baada ya kuweka ule mpira ikaonekana kama atapiga Abdul (Juma) ambaye pia ni mzuri, akamuangalia Aishi Manula alivyokaa naye, akakaa kama jogoo flani hivi ambaye anatafuta mtetea akiwa anataka kwenda kushambulia, lakini hakwenda kwa haraka akawaacha walinzi wa Simba wakatulia kabisa. Akajivuta kutoka kwenye nyuzi mduara kwenda kwenye nyuzi 33, 34 hivi akapiga semi banding block buster pin ball kwenda moja kwa moja na Manula amekuwa na shida hii mara kwa mara hakuuona mpira ule ulikuwa ni wa moto mnoo, kama ni vipimo kilomita 122 kwa saa.”

DUBE VS YANGA

Bao pekee la Azam na la ushindi dhidi ya Yanga katika dakika ya 86 kwenye mechi iliyopigwa Aprili 25, 2021 katika Uwanja wa Benjamin Mkapa nalo lilisimuliwa na Kashasha namna hii:

“Top striker huyo international Zimbambwe bonge la bao. Ni kama hivi mita zaidi ya 24, 26 nje ya penalt box, baada ya kupata asisti nzuri kutoka kwa Never Tigere long pass, akaangalia goli liko wapi hakutaka ku-drive, akanyooka akapiga mpira mmoja mzuri mno block buster, tripple block buster, mpira ambao kwa kweli kwa namna yoyote ile ulienda kwenye angle alikosimama Faroukh Shikhalo, lakini kwa ukubwa na uzito wa mpira ule hakuweza kuuona. Mpira ulikuwa kama unazunguka hivi spining ball, stand spining, lakini ni mpira uliokwenda umenyooka nyuzi 180 ukiwa umetoka usawa wa ardhi kwa maana ya precision, kama ni flight basi maana yake ni mita kama mbili na robo hivi toka usawa wa ardhi, ndio maana golikipa hakufikiria ku-punch wala kuulalia ukapita upande wake wa kulia ikawa ni kamba. Bonge la bao, Prince Dube, top striker, top scorer wa Azam FC...kwako Enock Bwigane kamarada.”

Mwalimu Kashasha alifariki dunia Alhamisi wiki hii wakati akiendelea kupatiwa matibabu katika Hospitali ya Hurbert Kairuki, Dar es Salaam kutokana na kusumbuliwa na tatizo la figo na pia ilielezwa alipatwa na maambukizi ya Uviko 19.

Columnist: www.mwanaspoti.co.tz