Magufuli Kukumbukwa kwa Kuinua Elimu March 31, 2021 by Global Publishers
RAIS wa Awamu ya Tano, Dk John Magufuli ametajwa kuwa mzalendo na shujaa aliyepania kulisaidia Taifa la Tanzania kwenda mbele kwa kasi kwa kuwasaidia watoto wa Kitanzania wanyonge kupata elimu bila malipo na kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia.
Kauli hiyo imetolewa na Mkuu wa Shule ya sekondari ya Mpwapwa mkoani Dodoma, Omary Tofiq akizungumzia anavyomkumbuka kiongozi huyo aliyefariki Machi 17 na kuzikwa Machi 26 mwaka huu.
Alisema kama kweli Watanzania wanataka kumuenzi na kumkumbuka Dk Magufuli wanatakiwa kutunza na kudumisha mazingira katika maeneo mbalimbali.
Mwalimu Tofiq alisema Shule ya Sekondari ya Mpwapwa ni miongoni wa shule kongwe hapa nchini ambayo iliianzishwa mwaka 1926 na serikali ya kikoloni ikiwa na lengo la kuwaandaa watoto wa machifu ambao watakuwa wasaidizi katika serikali ya kikoloni.
Alisema baada ya Rais Magufuli kuingia madarakani shule kongwe zilinufaika kwa kufanyiwa ukarabati mkubwa ambao umeleta matunda mengi na hasa hamasha kwa wanafunzi kusoma na walimu kufundisha hivyo kukuza kiwango cha elimu.
Shule hiyo ilipokea Sh bilioni 1.2 katika mwaka 2017/2018 ambazo zilisaidia shule hiyo kufanyiwa marekebisho ya mabweni, majengo ya utawala, madarasa na kujengwa kwa bweni jipya la wasichana.
Alisema pia shule hiyo ni ya kitaifa ambayo hujumuisha watoto wenye mahitaji malumu ambao kabla ya Dk Magufuli wanafunzi hao walikuwa wanakabiliwa na upungufu mkubwa na vifaa vya kujifunzia kama mashine za kuandikia na karatasi zake.
Aidha Mwalimu Omary alisema, kabla ya Mpango wa Elimu bila Malipo, wanafunzi wengi waliokuwa wanatoka katika familia za kimaskini walishindwa kumaliza masomo, lakini baada ya mpango wa elimu bila malipo kuanzishwa idadi ya watoto kutoka familia maskini wanamaliza masomo na wanafanya vizuri.
Mmoja wa wanafunzi wenye mahitaji malumu, Robert Kilumba alisema mazingira ya sasa ya kujifunzia, yameboreshwa na wameondolewa changamoto na hivyo sasa wanafanya vizuri katika mitihani yao.
Naye Ofisa Elimu Sekondari Wilaya hiyo, Nelson Milanzi alisema, baada ya shule hiyo kufanyiwa ukarabati imeweza kuongeza ari ya ufundishaji kwa walimu na wanafunzi kujisomea.
Milanzi alisema katika mtihani wa kidato cha sita shule hiyo ilitoa mwanafunzi mmoja aliyekuwa katika wanafunzi kumi bora waliofanya vizuri katika mtihani wa kidato cha sita mwaka 2020. Pia alisema katika mtihani wa kidato cha nne mwaka 2020, pia iliweza kuongoza kimkoa katika shule za sekondari za mkoa wa Dodoma.