Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

MAGUNOMICS: Sera za Magufuli zilizoleta mageuzi chanya kiuchumi

Bdeb1597287345426f13e54f45046d5d MAGUNOMICS: Sera za Magufuli zilizoleta mageuzi chanya kiuchumi

Fri, 19 Mar 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

NENO ‘Magunomics’ ni geni, lakini nimewiwa kulianzisha kwa kuwa linasawiri muktadha wa makala haya. Linatokana na maneno mawili: Magu ambalo ni kifupi cha Magufuli, aluyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa serikali ya Awamu ya Tano na nomics linalomaanisha economics au kwa Kiswahili uchumi.

Hivyo, andiko hili linatafsiri neno ‘Magunomics’ kama sera za mageuzi ya kiuchumi zilizotekelezwa na Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Magufuli.

Kama tunavyofahamu, Oktoba, 2015 Magufuli alichaguliwa kwa mara ya kwanza kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa Awamu ya Tano kwa kipindi cha miaka mitano (2015-2020) kabla ya kuchaguliwa tena Oktoba mwaka jana. Mara baada ya kuingia madarakani, Rais Magufuli alianza kutekeleza mageuzi makubwa ya kiuchumi ambayo hayajawahi kutokea katika historia ya Tanzania.

Lengo kuu la mageuzi hayo yalikuwa ni kujenga uchumi imara - uchumi wa viwanda - ambao ungeiwezesha Tanzania kufikia uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025 lakini tukafikia muda huo hata kabla ya muda. Ni uchumi uliolenga pia kupunguza umaskini na kuboresha maisha ya wananchi, kuiwezesha nchi kujitegemea na kutetea maslahi yake.

‘Magunomics’ ililenga kutekeleza mageuzi katika maeneo manne makubwa: Kujenga mahusiano yenye tija/manufaa na mataifa ya nje, kupambana na rushwa na ufisadi, kutekeleza sera za kibajeti za mapato na matumizi (kuongeza mapato ya serikali na kupunguza matumizi ya serikali yasiyo ya lazima) na kuwekeza kwenye miradi maalumu ya kimkakati ya maendeleo (hard and soft infrastructure) na sera za kifedha.

TANZANIA KABLA YA MAGUNOMICS

Wanazuoni wengi wanaamini kuwa ili uweze kuelewa hali ya sasa, ni muhimu kwanza kuelewa hali iliyopita.

Kwa maneno mengine, kwa kuwa hali ya nchi ya kiuchumi, kijamii na kisiasa ya sasa inategemea kile kilichofanyika wakati uliopita ndani na nje ya nchi, ni vyema sehemu hii ikaelezea kwa kifupi utekelezaji wa diplomasia ya uchumi na kile kilichokuwa kinafanyika ndani ya nchi kabla ya mageuzi.

Maelezo hayo kwa pamoja yatajenga msingi wa kuelewa vizuri kile kilichotekelezwa na serikali ya Awamu ya Tano.

Ni ukweli usiofichika kwamba Serikali za Awamu zilizopita zilifanya mambo mengi mazuri na makubwa. Mengi tuliyaona yakifanyika au yakiendelezwa hata kwenye serikali ya awamu ya tano kama ujenzi wa barabara, madaraja mtambuko (flyovers), ujenzi wa reli ya kisasa, upanuzi wa bandari na uwanja wa ndege ni mwendelezo wa msingi uliowekwa kwenye awamu zilizopita. Lakini pia alikuja na miradi yake mingi mipya kama ujenzi wa bwawa la Nyerere, ujenzi na boreshaji wa hospitali na vituo lukuki vya afya, mradi wa kuhamia Dodoma na kadhalika.

Hata hivyo, ni ukweli usiofichika pia kwamba awamu zilizopita ziliruhusu 'uholela' ambao uliosabaisha nchi kugubikwa na vitendo vya rushwa na ufisadi wa kutisha.

Utekelezaji wa Diplomasia ya Uchumi

Pamoja na kwamba kuna sababu nyingi zinazopelekea nchi moja kuingia kwenye uhusiano na nchi nyingine (uhusiano wa kimataifa), moja ya sababu muhimu ni ili iweze kutimiza matakwa/maslahi (interests) yake ya kiuchumi kupitia biashara, uwekezaji, utalii, misaada na kupokea teknolojia ya kisasa.

Kwa maneno mengine, tunaingia kwenye uhusiano wa kimataifa ili tuweze kunufaika kiuchumi. Sababu nyingine zote zinasaidia tu kufikia lengo hilo.

Kwa bahati mbaya, kwa miaka mingi, Watanzania hawajanufaika vya kutosha na uhusiano huo. Licha ya kuwa na uhusiano mzuri na nchi nyingi na uwingi wa rasilimali tulizonazo, Tanzania ilikuwa na imeendelea kuwa ‘shamba la bibi’ ambalo washirika kutoka nje walikuwa wakipora rasilimali zetu kwa kiwango cha kutisha!

Profesa Patrick Loch Otieno (PLO) Lumumba anaeleza hali hiyo kwa namna inayovutia na kueleweka vizuri zaidi. Anasema: "Kwenye meza ya chakula (mgawanyo wa mali/utajri wa dunia), kuna vitu vitatu: chakula cha kuliwa (food to be eaten), mlaji wa chakula (the dinner) na mhudumu wa chakula (the waiter).”

Kwa miaka mingi mnufaika katika meza hiyo ya chakula amekuwa mlaji wa chakula, hali mhudumu akihudumia walaji wa chakula na chakula kikiliwa na mlaji. Kwa maana hiyo, ‘kwenye meza ya chakula’, Tanzania imekuwa chakula cha kuliwa badala ya kuwa mlaji wa chakula.

Tanzania tumekuwa chakula cha kuliwa kupitia mikataba mibovu kwenye uvunaji wa rasilimali zetu na unyonyaji kupitia wanayoiita biashara ya kimataifa, uwekezaji na misaada ya maendeleo.

Maana yake ni kwamba, kwa miaka mingi uwekezaji, biashara ya kimataifa na misaada ya maendeleo imekuwa ikiendeshwa kwa manufaa/maslahi (interests) ya wawekezaji, wafanyabiashara wa nchi za Magharibi na watoa misaada badala ya kuwanufaisha wanaowekezwa, wafanyabiashara wa Tanzania na wapokea misaada (yani, Watanzania). Kwa kushirikiana na mataifa ya nje Watanzania tumekuwa tukiliwa kwa njia zifuatazo:

Uwekezaji

Mara nyingi wanaojiita wawekezaji wanataka faida kubwa (maximized profits) kupitia misamaha ya kodi, kutumia malighafi kutoka nchini kwao, kukwepa kodi, kuajiri wafanyakazi ghali kutoka nchi inayowekeza na kutumia teknolojia inayotumia mashine au mitambo (capital intensive) zaidi ya nguvukazi au misuli (labour instensive).

Wamekuwa pia wakiwekeza nchini mwao faida inayopatikana badala ya kwenye nchi walipowekeza na makampuni ya kigeni kufuata mipango ya maendeleo ya nchi zao badala ya mipango ya nchi wanapowekeza.

Biashara

Biashara ya kimataifa imekuwa ikitumiwa na nchi za Magharibi kama silaha ya kuwanyonya na kudumisha utumwa kwa mataifa ya Kusini hasa yale ya bara la Afrika. Unyonyaji na utumwa unaotokana na biashara ya kimataifa umekuwa ukifanyika kupitia makubaliano mbalimbali kama EPA na AGOA ambayo yanashurutisha kuwepo kwa biashara huru, kuondoa vikwazo vya kibiashara kwenye masoko ya ndani na mabadilishano ya bidhaa na huduma yasiyo sawia.

Nchi za Kusini zimekuwa zikilazimishwa kukubali kusaini makubaliano hayo, vinginevyo zinatishiwa kunyimwa misaada ya maendeleo kutoka nchi za Magharibi na pengine kuwekewa vikwazo vya kiuchumi.

Misaada

Misaada mingi imekuwa na mikakati ya kutekeleza mipango ya maendeleo ya wafadhili ambayo inaweza kutofautiana na ile ya nchi inayopokea misaada. Pia, misaada imekuwa na masharti mengi kama vile kuajiri wataalamu ghali na kununua malighafi kutoka nchi misaada inakotoka, kukwepa kodi kwenye miradi waliyowekeza na kutorosha fedha.

Masharti mengine ni kulazimisha kukubali mambo kama ya ushoga, kupokea kama kasuku aina ya demokrasia ya nchi za Ulaya na haki za binadamu, masharti ambayo mara nyingi yanawanufaisha watoaji wa misaada badala ya wapokeaji.

Hali ilivyokuwa ndani ya nchi

Watanzania wengi wanaamini kwamba baadhi ya viongozi wa serikali za Awamu zilizopita walikuwa legelege, waoga na ambao hawakuwa na uthubutu wa kuwawajibisha walio chini yao.

Matokeo yake, Tanzania - kitaifa na kimataifa - ilikuwa ‘shamba la bibi’ ambalo kila mtu alijichumia alivyopenda. Ilifika wakati uovu ulizagaa mpaka ‘huko’ yanapofanyika maamuzi na mafisadi walitumia madaraka kutoka ‘huko’ kuendeleza ufisadi wao. Mafisadi walitafuta uongozi na kuingia kwenye majukwaa ya maamuzi si kwa sababu ya uwezo wao au dhamira zao njema bali kuendeleza ukwasi, ubinafsi na uchoyo wao!

Ndiyo maana Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere aliwakumbusha kwamba "ikulu ni mahali patakatifu" na wote wanaotaka kuongoza taasisi hiyo muhimu lazima wawe watakatifu.

Kwa hali ilivyokuwa, nashawishika kuamini kwamba ama viongozi wenyewe au ndugu zao au wake zao au rafiki zao au waliowaweka madarakani walikuwa ndiyo ‘wapigaji’ wenyewe.

Haiingii akilini kabisa kwamba wapiga madili wakubwa walikuwa wanajulikana lakini wengi wao hawakuguswa. Na wachahe walioguswa walihamishwa kutoka kazi moja kwenda nyingine au mkoa mmoja kwenda mwingine au waliachishwa kazi kama njia ya kupewa likizo kwenda ‘honey money’ ili wakatafune fedha walizopora kwa amani.

Watanzania wengi waliamini kwamba viongozi wengi walikuwa hawajui tunataka kwenda wapi na tutafikaje tuendako. Viongozi wa aina hiyo ni hatari kwa maendeleo ya nchi. Ndiyo maana licha ya kuwa na rasilimali nyingi nchi ilibaki kwenye hali ya kuaibisha!

Itaendelea Jumatatu

Profesa Kitojo Kagome Wetengere ni mchumi na mshauri binafsi wa masuala ya uchumi, hususani katika eneo la Diplomasia ya Uchumi.

Columnist: www.habarileo.co.tz