Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

Katazo za Tamisemi vyeti vya chekechea ni jema

D5bffba1389f1538da4286f12e90aa13.png Katazo za Tamisemi vyeti vya chekechea ni jema

Wed, 5 May 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mamlaka za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Ummy Mwalimu, amenukuliwa akizipiga marufuku shule za msingi nchini kudai cheti cha kuhitimu elimu ya awali kwa watoto wanaotaka kuanza darasa la kwanza.

Alitoa marufuku hiyo bungeni juzi wakati akijibu swali la msingi la Mbunge wa Viti Maalum, Mariam Kisangi (CCM), aliyetaka kujua majibu ya serikali kutokana na kuwepo kwa sharti la watoto wanaotaka kuandikishwa darasa la kwanza kutakiwa kuwa na cheti cha kuhitimu elimu ya awali (chekechea) hasa kwa Mkoa wa Dar es Salaam.

Kimsingi, ingawa muuliza swali aliutaja hasa Mkoa wa Dar es Salaam, kwa kuwa tatizo hilo labda ni kubwa zaidi huko, ukweli ni kwamba kasumba ya walimu

wakuu wa shule za msingi na wasaidizi wao kuwadai watoto wanaotaka kuanza elimu ya msingi yaani, darasa la kwanza, ipo si tu kwamna lipo Dar es Salaam pekee, bali hata katika mikoa mingine.

Majibu na katazo la Waziri Ummy yanabainisha kuwa, ama kwa makusudi au kwa kutokujua, walimu hao katika shule za msingi wamekuwa wakifanya kosa ambalo pengine, limewafanya watoto wengi kuchelewa kuanza kufaidi haki hiyo ya kupata elimu eti kwa kuwa, hawakusoma na hawana vyeti vya kusoma na kuhitimu katika shule za awali.

Ndiyo maana Waziri Ummy ananukuliwa akisema: “Ni marufuku kwa shule kudai ‘certificat’ ya awali kwa wanafunzi wanaoanza darasa la kwanza. Ninachotaka kusema, bado

hatujafanya vizuri kuongeza ‘access’ ya watoto kuanza elimu ya awali, kwa hiyo haileti mantiki kusema kila mtoto anaeanze darasa la kwanza, awe na certificate ya awali.”

Akaweka wazi akisema: “Wote wanaodai certificate ya elimu ya awali kwa watoto hao, wajue wanatenda kinyume na maelekezo na miongozo ya serikali.”

Kimsingi, katazo hili la waziri ni jema kwa kuwa si siri, madai ya cheti hicho yameathiri watoto wengi na pengine, yamekuwa yakitumika kama moja ya vyanzo vya mapato yasiyo halali ya walimu hao kwa kuwa yanatengeneza mazingira ya kudai na kupokea rushwa kwa kutoka kwa wazazi.

Ninasema hivyo kwa kuwa uzoefu katika jamii unaonesha kuwa, wazazi na watoto wengi hupata vipindi vigumu hasa wakati wa kuandikisha watoto kuanza darasa la kwanza, au kujiunga na kidato cha kwanza katika shule mbalimbali maana hapo, ndipo hubanwa kwa masharti mbalimbali halali na haramu ikiwamo hata michango iliyokatazwa na serikali.

Ndiyo maana ninasema, katazo hili la Wizara ya Tamisemi, ni jema, lizingatiwe na kufanyiwa kazi ili watoto ambao hawajapitia chekechea, wasinyimwe wala kucheleweshewa haki yao ya kuanza elimu ya msingi.

Columnist: www.habarileo.co.tz