Ilikuwa kwangu ngumu, kuamimi jambo hili
Kwamba rubani muhimu, Joni Pombe Magufuli
Keshaiaga kaumu, roho imeacha mwili
Nenda baba Magufuli, kweli chema hakidumu.
Wallahi nilitamani, habari isiwe kweli
Mama Samia Hasani, aikanushie mbali
Kwamba ni mitandaoni, wamemlisha kauli
Nenda baba Magufuli, kweli chema hakidumu.
Japo ni ngumu kumeza, nimesadiki ukweli
Kwamba yarabi muweza, keshalitwaa jabali
Tangu sasa hatoweza, kuwa na sisi kimwili
Nenda baba Magufuli, kweli chema hakidumu.
Ghafla iso hiari, jembe meondoka kweli
Nafikiri sibashiri, takuwaje zetu hali
Alitujaza jeuri, nchi hii ni asali
Nenda baba Magufuli, kweli chema hakidumu.
Neema tulishaona, zikitiririka tili
Na uchumi ukinona, ukisonga kwenda mbali
Kichwa kinauma sana, naona giza kwa mbali
Nenda baba Magufuli, kweli chema hakidumu.
Ile kansa ufisadi, aliondoshea mbali
Wanyonge wakafaidi, kwa huduma mbalimbali
Akasimika miradi, ni muhimu kweli kweli
Nenda baba Magufuli, kweli chema hakidumu.
Kwa nini tulikupenda, vile ni mtu mkweli
Wajua tulikupenda, vile ni mtu adili
Hakika tulikupenda, wanyonge yako madili
Nenda baba Magufuli, kweli chema hakidumu.
Fununu zilipokuja, kwamba una ngumu hali
Wenye nia ya pamoja, tuliomba kwelikweli
Mungu akupe faraja, urejee njema hali
Nenda baba Magufuli, kweli chema hakidumu.
Rabi ungetuuliza, tungekwambia ukweli
Kwako tungependekeza, mpe tisini kamili
Atuache twapendeza, tukijilia vidali
Nenda baba Magufuli, kweli chema hakidumu.
Mwenyezi mlaze pema, John Pombe Magufuli
Ile siku ya kiama, mlipe kwa maadili
Ingawa ametuhama, tutamkumbuka kweli
Nenda baba Magufuli, kweli chema hakidumu.