Kadri wakati unavyopita, teknolojia imeendelea kukua na kuibua aina mpya za mawazo kuhusu mawasiliano. Maendeleo ya teknolojia yamebadilisha jinsi mawasiliano yanavyofanyika. Watafiti wamegawanya jinsi mawasiliano yalivyobadilika katika hatua tatu;-
Mabadiliko ya mwanzo: Mawasiliano ya kwanza katika maandishi yalianza na michoro. Maandishi hayo yaliandikwa kwenye mawe ambayo yalikua mazito mnoo kuhamishwa. Wakati huo mawasiliano ya maandishi yasingeweza kubebwa, ingawa yalikuwepo.
Mabadiliko ya pili: Maandishi yalianza kufanyika kwenye makaratasi,mavunjo,na udongo n.k herufi za alfabeti zilibuniwa hivyo basi kuruhusu mfanano wa lugha katika maeneo makubwa.
Mabadiliko ya tatu: Taarifa inaweza kuhamishwa sasa kupitia mawimbi na ishara za kielektroniki. Nguvu ya teknolojia katika kubadilisha utaratibu wa maisha ya dunia ni kubwa zaidi na lilikuwa suala la muda tu kabla ya kila aliye chini ya jua kukubaliana na mapinduzi haya.. Matumizi ya teknolojia yalianza tangu karne ya 19 ulimwenguni, lakini ubadilishaji wa mifumo ya uendeshaji kutoka mifumo ya analojia kwenda dijitali ilikawia.
Nchi zilizoendelea zilishapiga hatua za mabadiliko ya kidijitali tangu miaka ya 2000, huku biashara na kampuni nyingi zikibadilisha uendeshaji wao kuwa wa kidijitali kuanzia mwaka 2010 na kuendelea.
Hapa nchini baadhi ya taasisi, nyingi zikiwa binafsi, zilishanusa fursa hiyo na kuamua kwenda dijitali kwa haraka na tuliona namna zilivyofanikiwa kwa kiasi kikubwa hata katika mapambano dhidi ya Ugonjwa wa Uviko-19.
Kwa upande wa Serikali, taasisi nyingi za umma zilikuwa bado zikijiendesha kianalojia kwa kuwa Serikali yenyewe bado haikuwa imeiingia rasmi katika mabadiliko hayo, isipokuwa chache kama vile Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) ambayo kulingana na asili ya kazi zake iliilazimu kwenda huko mapema zaidi. Tunaona mawasiliano ni muhimu kama mfumo wa mishipa ya fahamu ya uchumi wa nchi hasa katika kipindi hiki ambacho nchi nyingi zinajenga uchumi wa kidigitali,mawasiliano yanakua ndiyo moyo wa uchumi wa jamii.
TCRA ilianzishwa kama chombo cha usimamizi wa mawasiliano baada ya kuonekana kuna umuhimu wa usimamizi wa njia za mawasiliano ili kuwa na matumizi sahihi ya mawasiliano kwa maendeleo ya taifa na TCRA imeweza kutoa huduma kwa zaidi ya miaka 17 toka ianzishwe na imefanya kazi yake kwa ufanisi wa hali ya juu ikizingatia mabadiliko ya TEHAMA. Azma ya Rais Samia Suluhu Hassan
Ikimbukwe kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan mara baada ya kuingia madarakani, moja ya mambo aliyoyawekea msisitizo ni kuifanya Tanzania ya kidijitali na kuinua nchi na kuiweka kwenye mipaka mipya ya TEHAMA.
Zaidi, akitaka mkongo wa Taifa wa mawasiliano kuimarishwa na maeneo mengi kufikiwa na huduma za mawasiliano.
Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anasisitiza asilimia 40 ya maeneo ya umma kuwa na mawasiliano ya masafa ya kasi katika kipindi cha miaka mitano ijayo na ameainisha maeneo 19 ya kimkakati kuimarisha mawasiliano kuelekea katika uchumi wa kidijitali.
Maeneo hayo ni pamoja na kuongeza mchango wa sekta ya mawasiliano katika pato la Taifa (GDP) kwa kuongeza matumizi ya Tehama, kubuni na kutekeleza mikakati ya kuweka mazingira bora ya ushindani na udhibiti katika sekta ya mawasiliano ili wananchi wengi wamudu gharama na kuongeza wigo na matumizi ya mawasiliano ya kasi kutoka asilimia 45 mwaka 2020 kufikia 80 mwaka 2025.
Mengine ni kuongeza watumiaji wa intaneti kutoka asilimia 48 mwaka 2020 hadi kufikia asilimia 80 mwaka 2025, kuanzisha huduma za mawasiliano za intaneti ya kasi katika maeneo ya umma yakiwamo maeneo ya hospitali, taasisi za elimu na vituo vya usafiri hadi kufikia asilimia 40 mwaka 2025 na kuendeleza Serikali Mtandao inayozingatia usalama wa mifumo na taarifa za Serikali.
Sambamba na jitihada hizo, pia Serikali hii ya Mama Samia, inakusudia kurahisisha utoaji huduma mbalimbali za Serikali kwa umma kwa kuanzisha vituo vya huduma ili kuongeza ufanisi na kurahisisha upatikanaji wa huduma za Serikali. Lengo likiwa ni kuwarahisishia watumishi wa umma utendaji kazi wao na kuwapatia wananchi huduma kwa urahisi na ufanisi.
Kama hiyo haitoshi, pia uunganishaji wa miundombinu ya mtandao wa kasi mkononi ili kupatikana maeneo yote ya kuweka mazingira wezeshi ya kuanzisha viwanda vya uzalishaji wa vifaa vya Tehama vyenye uwezo wa kutoa ajira kwa wananchi walio wengi na kuzalisha vifaa vilivyotumika ndani na nje ya nchi, kufanyika. Ujenzi wa viwanda vya kuchakata taka za kielektroniki ili kudhibiti uharibifu wa mazingira.
Mipango ya kuiwezesha Tanzania kuwa na uchumi wa kijigitali ni pamoja na kurahisisha utoaji wa huduma mbalimbali za serikali kwa umma kwa kuanzisha vituo vya Huduma za pamoja (One Stop Centres) ili kuongeza ufanisi na kurahisisha upatikanaji wa huduma za Serikali aidha, inakusudia kuimarisha Serikali mtandao inayozingatia usalama wa mifumo na taarifa za Serikali na kuwarahisishia watumishi wa umma utendaji kazi na wananchi kupata huduma kwa urahisi na ufanisi zaidi.
TCRA na uekelezaji wa azma hiyo
Ikiwa ni taasisi inayosimamia masuala ya mawasiliano nchini, TCRA imekuwa mstari wa mbele kutekeleza azma hiyo ya Serikali ambayo kwa sasa ndiyo kipaumbele katika sekta ya mawasiliano.
Mamlaka hiyo imeweka bayana mpango wa kuwawezesha vijana wabunifu katika Teknolojia ya Habari na Mawasiliano kuibua bunifu nyingi zaidi zitakazonufaisha uchumi wa nchi. “Tupo kwenye zama za kidijitali; kwa hiyo mawazo na fikra kwa jinsi walivyo hawa vijana ni tofauti na kipindi cha nyuma, vijana wanafikiri na kuona vitu tofauti, kwa hiyo ni lazima tuweze kupata mambo mengi kutoka kwao (vijana)” anasisitiza Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, Dk Jabiri Bakari.
Pia, anaeleza kuwa kama mamlaka imejikita kutumia mifumo hiyo ya Tehama katika kuleta mabadiliko ya kidijitali ili kuweza kufikia lengo la ‘Unganisha 2030’ ambapo mifumo hiyo na ya mawasiliano kwa pamoja utaharakisha maendeleo ya kiuchumi.
Maeneo mengine ni kupanua huduma za mawasiliano za intaneti ya kasi katika maeneo ya umma hadi kufikia asilimia 40 mwaka 2025 na kuendeleza serikali mtandao inayozingatia usalama wa mifumo na taarifa za serikali.
Mkazo pia uko kwenye kuendeleza miundombinu ya mawasiliano ili kuiwezesha kupitisha mawasiliano yanayotumia masafa ya kasi, teknolojia mpya, huduma za posta na maudhui ya utangazaji ya ndani.
Vilevile, TCRA imeendelea kuratibu utekelezaji wa mfumo wa kitaifa wa anwani na postikodi, kuhimiza upatikanaji wa huduma za mawasiliano kwa wote na kuweka misingi ya matumizi ya teknolojia mpya.
TCRA, katika utekelezaji wa azma hiyo, inasimamia usalama mitandaoni kupitia Kituo cha Kitaifa cha Mwitikio wa Kukabiliana na Majanga ya Kompyuta (TZ—CERT), Sheria ya Makosa Mtandaoni (Cybercrime Act, 2015) na uendeshaji wa shindano la usalama mtandaoni.
Dk Bakari, anasisitiza kwamba ni muhimu kwa upande wa wananchi wakashirikiana na mamlaka pamoja na serikali kwa ujumla kwa kutoa taarifa za wahalifu wa mtandaoni kwa kutuma ujumbe na namba za washukiwa wa utapeli kwenda namba 15040 ili kutoa taarifa yavitendo hivyo kwa shabaha ya kutokomeza vitendo vya uhalifu kwenye mtandao.
Mashuhuda
Kwa kuwa mabadiliko haya ya kidijitali ni jambo lenye tija kwa Watanzania wengi baadhi yao wanaeleza kwa ufupi namna uendeshaji wa shughuli zao ulivyoimarika tangu kuyapokea mabadiliko hayo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Maktech, Godwin Makyao anasema kuwa kampuni yake imewekeza vya kutosha katika teknolojia za Tehama ili kuweza kuongeza ufanisi wa shughuli za kampuni hiyo. Anasema anaona bado kuna fursa ya vijana wa Kitanzania kuvumbua teknolojia mpya kwani asilimia kubwa ya zilizokuwapo ni za kutoka nje ambazo uendeshaji wake ni wa gharama kubwa kuliko kama ikizalishwa hapa ndani.
Kwa upande wa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (Osha), Khadija Mwenda anasema kutokana na changamoto mbalimbali za kiutendaji zilizokuwa zinaikumba taasisi kwa muda mrefu mathalani taasisi kushindwa kutoa huduma bora, ukosefu wa taarifa sahihi kwa wakati mwafaka, upotevu wa maduhuli ya Serikali, ufanisi mdogo katika utekelezaji wa majukumu ya Taasisi, changamoto katika kufanya usuluhishi wa mahesabu (reconciliation), ndiyo yaliyowasukuma kuanza kufikiri ni kupitia njia ipi watajikwamua kutoka katika changamoto tajwa.
“Sambamba na changamoto tajwa, safari hii ya kidijitali ilichagizwa na agizo la Serikali lililozitaka Taasisi zote za udhibiti kufanya maboresho katika utendaji ili kukuza biashara na uwekezaji nchini.
Agizo hilo lilitolewa baada ya Serikali kufanya tathmini ya mifumo ya udhibiti wa Biashara na Uwekezaji ambayo ilikuja na andiko maalum (Blue Print) lililoainisha vikwazo katika sekta ya biashara na uwekezaji na kutoa mapendekezo ya namna ya kuviondoa vikwazo hivyo.
Miongoni mwa mapendekezo yaliyokuwemo katika andiko ilikuwa ni kuzitaka taasisi za udhibiti kuboresha huduma zake kupitia kusimika mifumo mbalimbali ya Tehama,” amesema Bi Mwenda.
Naye Mkuu wa Kitengo cha Tehama na Takwimu wa Brela, Enock Chanya anasema kuwa, “Safari yetu ya mabadiliko ilianza muda mrefu takribani miaka mitano iliyopita, ambapo mifumo ilianza kufanya kazi na kufanyiwa maboresho mara kwa mara kutokana na mabadiliko ya teknolojia.
Ili kuendana na mabadiliko ya teknolojia tumeendelea na tutaendelea kufanya maboresho kwa mifumo iliyopo na kuanzisha mifumo mipya ili kuongeza ufanisi zaidi katika utoaji wa huduma zetu.”
Hitimisho
Dk Bakari anabainisha kuwa TCRA inaweka mazingira wezeshi kuhakikisha sekta ya Mawasiliano inakuwa na mchango mkubwa katika ukuaji wa uchumi wa nchi kuendana na azma ya nchi ya Tanzania ya Kidijitali.