Winga Dikson Ambundo kama mnamchukulia poa atawaumiza, na kocha wake mapema kasema huyu ni mtu ambaye anajua anachokifanya uwanjani hasa akishika mpira.
Ambundo ambaye amesajiliwa na Yanga msimu huu akitokea Dodoma Jiji, jamaa amekuwa na moto mkali akiwa na pasi za uhakika kila anaposhika mpira huku pia kasi yake ikiwa sio ya kubahatisha.
Katika mazoezi ya jana nusura amfanye kitu kibaya beki Paul Godfrey ‘Boxer’ baada ya kumtingisha na jamaa akatingishika, kisha akapiga pasi moja ya hatari tukio ambalo liliamsha shangwe kwa wenzake.
Baada ya tukio hilo kocha Nasreddine Nabi alikuwa akifuatilia akabaki anacheka tu kisha akamwabia “safi sana kijana endelea kukimbiza.”
Baaada ya mazoezi Nabi amesema Ambundo ni mmoja kati ya wachezaji ambao wamemkosha kwa uwezo wake akiwa ni hatari anaposhika mpira na kuelekea langoni.
Kocha huyo amesema winga huyo mzawa kama ataendeleza moto atafanya makubwa katika kikosi chake ambapo ubora wake umemkosha na anategemea makubwa zaidi.
“Ni mchezaji jasiri sana anaposhika mpira hasa anapomfuata beki, nimemuona akiwa anacheza mechi, lakini sasa naona ni hatari zaidi baada ya kumuona akiwa hapa nasi akiendelea hivi atasumbua,” amesema Nabi.