Hoja ya kufutwa au kutofutwa kwa sheria ya kunyongwa bado
Na Matern Kayera
SERIKALI imesema hakuna mjadala hivi sasa kuhusu kufutwa au kutofutwa kwa sheria ya kunyongwa.
Hayo yalibainishwa na Katibu Mkuu Wizara ya Katiba na Sheria, Profesa Sifuni Mchome alipozungumza jana na HabariLeo.
Baada ya Rais John Magufuli kutangaza kuwapunguzia adhabu wafungwa 256 waliopaswa kunyongwa na kuagiza wafungwa hao wafungwe maisha, HabariLeo lilitaka kufahamu kama baada ya uamuzi huo wa Rais kuna mpango wowote wa serikali kupeleka hoja Bungeni ili kubadilisha sheria ya kunyonga ili iwe kifungo cha maisha au vinginevyo.
Profesa Mchome alisema hivi sasa mjadala kuhusu kufuta sheria hiyo ya kunyonga haupo na Rais Magufuli alisema wengine watakaokuja baada yake wakitaka waendelee kunyonga.
Desemba 9 mwaka huu ambayo ilikuwa siku ya Maadhimisho ya Miaka 59 ya Uhuru wa Tanzania Bara na siku ambayo Rais Magufuli aliitumia kuwaapisha Mawaziri na Naibu Mawaziri aliowateua, pamoja na mambo mengine, aliwapunguzia adhabu wafungwa 256 waliotakiwa kunyongwa katika kipindi cha miaka mitano ya utawala wake.
Badala ya kutekeleza hukumu hiyo ya kuwanyonga, Rais Magufuli aliwapunguzia adhabu na kuagiza wafungwe maisha.