Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

Hatua za haraka zinahitajika kuzuia vurugu viwanjani

1563e2ed939196324f7d4593d89dfb9c Hatua za haraka zinahitajika kuzuia vurugu viwanjani

Mon, 5 Oct 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

TANZANIA ni miongoni mwa nchi chache duniani zilizoamua kuendelea na shughuli zake zikiwemo za kimichezo baada ya kujiridhisha kuwa maisha yanaweza kuendelea baada ya kupungua kwa maambukizi ya virusi vya corona.

Kwa takribani miezi mitatu dunia ilikuwa kwenye taharuki ya ugonjwa huo ambao umewapata mamilioni ya watu na kuua wengine wengi duniani kote. Kwa Afrika Mashariki, Tanzania ndio nchi pekee ilirejea kwenye maisha yake na hatimaye ligi mbalimbali zikaanza kuchezwa.

Kwa maana hiyo nchi jirani zote zimeelekeza macho yao Tanzania kuona mambo yanavyokwenda na kwa wale wapenzi wa michezo hasa soka wamekuwa wakiifuatilia Ligi Kuu Bara kwa karibu zaidi.

Kwa hali hiyo, badala ya Watanzania mashabiki wa soka kuendeleza upendo na ustaarabu ili kuzidi kuvutia majirani, wamekuwa watu wa kupigana na kuumizana bila sababu za msingi viwanjani.

Kwa zaidi ya mwezi sasa, matukio ya uvunjifu wa amani yametokea mara mbili, kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam na ule wa Jamhuri, Morogoro. Kote huko inadaiwa mashabiki wa Yanga wanawapiga mashabiki wa Simba kwa sababu ambazo hazijawa bayana.

Kwa nyakati tofauti, uongozi wa Yanga, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) na Simba umetoa matamko kukemea matukio hayo.

Kwanza, tunalaani matukio haya kwa sababu hayaleti picha nzuri mbele ya macho ya dunia na yanaondoa ile dhana ya kuwa michezo ni furaha na upendo na inasaidia katika kujenga umoja na mshikamano katika jamii.

Mashabiki wanatakiwa kufahamu jinsi Ligi Kuu ya Bara inavyofuatiliwa na kukubalika nchi mbalimbali za Afrika Mashariki na Kati, hivyo wanapaswa kuwa watulivu viwanjani na kuepuka maafa kama yaliyowahi kutokea katika nchi nyingine duniani.

Ni kwa msingi huo tunazitaka klabu hizi mbili kongwe nchini za Simba na Yanga kuwakemea mashabiki wao na kuchukua hatua kali dhidi ya wote wanaohusika kuchochea vurugu hizo.

Aidha, TFF na Bodi ya Ligi zitumie kanuni zao kuchukua hatua za haraka za kudhibiti vurugu hizi viwanjani ili iwe funzo kwa mashabiki wengine wenye tabia kama hizo.

Tunaamini hatua hizi zitachukuliwa haraka kwa sababu tabia hii inaonekana inaanza kuota mizizi miongoni mwa mashabiki wa soka nchini jambo ambalo baadaye litakuwa gumu kulidhibiti.

Columnist: habarileo.co.tz