Kijamii

Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Lifestyle

SIL

MenuKijamiiMaoni
Articles

EAC shirikianeni kudhibiti ajali

573ff7ca72803e8f6494091a79a81283 EAC shirikianeni kudhibiti ajali

Tue, 24 Nov 2020 Chanzo: habarileo.co.tz

WIKI iliyopita kulifanyika maadhimisho ya siku kuwakumbuka waathirika wa ajali za barabarani na kuonekana kuwa watu wengi wamepoteza maisha kutokana na ajali hizo katika nchi za Afrika Mashariki na bado watu zaidi wanaendelea kufa.

Licha ya kila nchi kuweka mikakati mbalimbali, ikiwemo kutungwa kwa sheria mbalimbali kwa lengo la kupunguza vifo hivyo ambavyo sababu kubwa zinaweza kuzuilika, bado hali inazidi kuwa si nzuri.

Ajali hizo zimeendelea kugharimu maisha ya nguvukazi huku ikielezwa vyanzo vikuu vinavyochangia ajali hizo kuwa ni ubovu wa magari, makosa ya kibinadamu, mazingira ya barabara na vyanzo vingine.

Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani, Fortunatus Muslimu anasema katika kipindi cha mwaka 2010 na 2014 vifo vilikuwa 19,294 huku mwaka 2015 hadi 2019, vifo hivyo vikipungua na kufikia 12,533 sawa na asilimia 35.

Kuhusu idadi ya majeruhi, Muslimu anasema mwaka 2010 hadi 2014, majeruhi walikuwa 96,788, huku mwaka 2015 hadi 2019, idadi hiyo ikipungua na kufikia 30,410 sawa na asilimia 68.6.

Nchini Uganda, kuanzia mwaka 2018 mpaka mwaka huu vimeongeza vifo kwa asilimia tano kutoka matukio 3,500 katika mwaka 2018 mpaka 3,880 mwaka 2019.

Mkurugenzi wa Usalama barabarani, Charles Ssembambulide anasema kwa wastani, takribani watu 10,000 wanajeruhiwa kila mwaka kwa kuvunjika viungo huku wengine wakipata majeraha ya kudumu katika uti wa mgongo na kuwaathiri maisha yao yote na kuwa idadi ni kubwa kwani kuna taarifa nyingine haziwafikii.

Nchini Kenya, watu zaidi ya 3,114 wamefariki kutokana na ajali za barabarani mwaka huu na kufanya kuwa na ongezeko la vifo tofauti na mwaka jana ambao waliokufa watu 2,942.

Takwimu za Mamlaka ya Kitaifa ya Uchukuzi na Usalama (NTSA) zilizotolewa wiki iliyopita zinaonesha kuwa, matukio ya ajali yameongezeka kwa asilimia 5.8 na sababu zake zikiwa mwendo kasi, uendeshaji mbovu, huku kuendesha dereva akiwa amelewa.

Takwimu zinaonesha kati ya watu 4,571 waliojeruhiwa, 954 walikufa, 2,040 walijeruhiwa vibaya na 1,577 kupata majeraha ya kawaida.

Nchini Rwanda imebainika kuwa matukio ya ajali yamepungua kwa asilimia 17 kwa ajali za barabarani kwa mwaka jana ambapo watu 223 walipoteza maisha mwaka 2019 ukilinganisha na watu 465 waliopoteza maisha mwaka 2018.

Kwa wastani kwa mwaka mmoja au zaidi utabaini kuwa ajali za barabarani bado ni changamoto kubwa kwa kila nchi kwani licha ya kugharimu serikali fedha nyingi kwa ajili ya matibabu ya majeruhi kumekuwa na uharibifu wa vyombo vya usafiri.

Pia nchi hizo zinakosa nguvukazi kwa wale waliojeruhiwa kabisa kama kuvunjika uti wa mgongo na kuwa tegemezi, kusababisha ulemavu wa kudumu na hata vifo kwa wananchi wengi ambao wana mchango mkubwa kwa Taifa.

Ni vema sasa nchi za EAC kama wanavyoshirikiana katika masuala ya mapato, afya, uchukuzi na mengineyo, kuweka mkazo kwenye hili kwani linagharimu maisha ya watu wengi ikiwamo kutunga sheria ngumu au kutumia teknolojia kudhibiti madereva wakorofi.

Kama wahenga wanavyosema ‘kidole kimoja hakivunji chawa‘ hivyo kila nchi imekuwa na sheria na taratibu zake za kudhibiti ajali lakini bado hata kwa nchi ambazo ajali zimepungua idadi ya wanaokufa na wanaojeruhiwa bado iko juu.

Hivyo kwa kutumia uzoefu kwa kila nchi, ni vema nchi za EAC kukaa kwa pamoja na kutafuta mwarobaini wa tatizo hili la ajali katika ukanda huu ikibidi hata kushauriana kwa kubadilisha sheria za nchi kuhusu masuala ya usalama barabarani.

Columnist: habarileo.co.tz